MTANDAO WA
JINSIA (TGNP}
KITINI CHA UENDESHAJI WA URAGHIBISHI
GUIDELINE FOR CONDUCTING
PARTICIPATORY ACTION RESEARCH (PAR)
SEHEMU YA KWANZA.
Maana ya urgahbishi.
Uraghbishi hutegemea imani kubwa kuhusu uwezo na uelewa wa watu.
Uraghbishi unajengwa katika mtazamo alionao mraghbishi juu ya watu wengine kwa
kuwaona na kuamini kwamba wana maarifa ya kutosha, uelewa kuhusu hali zao na
uwezo hivyo wanahitaji kuchokozwa waweze kutafakari zaidi, kuchambua na
kuchukua hatua. Mraghbishi anawawezesha watu kujifahamu wenyewe na kujiamini
kwamba wanao uwezo mkubwa na ‘raghba’ yao hutokana na hali ya kujifahamu na
kujiamini.
Misingi ya uraghbishi na sifa za mraghbishi.
§ Kiu ya haki
kwa wote, hasa wale ambao wamenyanyaswa, au kukandamizwa au kunyonywa au
kupuuzwa au kusahauliwa na kutengewa na mfumo
§ Imani
kwamba binadamu wote wana uzoefu na ubunifu wao na hamu ya kuona kwamba uwezo
na ubunifu huu unapewa uzito unaostahili
§
Kupenda kutumia ushiriki wa hali ya juu
§ Uwezo wa
kuwachokoza watu ili waweze kuchambua hali halisi inayowakabili na mbinu za
kuibadili hadi wachuke hatua wenyewe
§
Uwezo wa kuwasiliana na watu na kuwawezesha kama mwenzao
§
Uwezo wa kujenga muafaka na maisha na kazi ya wale anaofanya kazi nao
§
Uwezo wa kukabili hali ya migogoro na hata ugomvi
Aina za uraghbishi.
Kwa kuzingatia
kwamba uraghbishi kweli ni mchakato kuliko tendo, yafaa kukumbuka kwamba
shughuli nyingine zinaweza kutumia falsafa na mbinu za uraghbishi, lakini si
uraghbishi kamili.
Uraghbishi kamili (mraghbishi wa ndani)
Katika
uraghbishi kamili, mtu (mtumishi wa ugani, mwanaharakati, au mgeni yeyote
anaenda kuishi katika jamii ambapo anataka kufanya uraghbishi. Huu ni
uraghbishi kamili kwa sababu unapotembelea jamii, au hata kuendesha mafunzo
huwezi kuelewa hali halisi ya jamii na wanajamii kwa muda mfupi hivyo. Aidha,
inachukua muda kwa jamii kumwelewa mraghbishi, kumpima na kumwamini ili
wajisikie huru kujadiliana naye.
Uraghbishi wa kutembelea (mraghbishi wan je).
Hapo
mwanaharakati, mtumishi wa ugani au mgeni yeyote anaingia na kutoka katika
jamii, mara nyingi kwa sababu hana muda. Hivyo hakai pale bali anaenda mara kwa
mara (na mara nyingine anaishi karibu pia). Huu si uraghbishi kamili na kwa
sababu mtu hana muda wa kutosha kuelewa na kueleweka, ni rahisi sana kurudia
tena mbinu za uhamasishaji na kutoa ushauri bila kuelewa kwa undani. Au kwa
sababu muda ni mfupi, ni rahisi kufikia kwenye maelezo badala ya maulizo, hasa
kama mraghbishi hana subira.
Uraghbishi wa mafunzo/warsha
Huu nao hauwezi
kuitwa uraghbishi kamili lakini mwezeshaji anaweza kutumia mbinu shirikishi na
za kiraghbishi zaidi katika kuendesha warsha. Hivyo daima hataanza na mihadhara
n.k. bali atajaribu kuwachokoza washiriki waseme walicho nacho wao na kujenga
juu ya wanavyoona wao.
Katika
uraghbishi wa aina zote, lengo kuu ni kuwahuisha, kuwazindua watu waweze
kushika usukani wa maendeleo yao na maisha yao, waweze kuchambua na kuelewa kwa
undani.
Hatua za uraghbishi.
Ili uraghbishi uweze kutimia kwa ukamilifu, inatakiwa hatua kuu tatu
muhimu lazima zipitiwe. Hatua hizi zinamwezesha mraghbishi na wanajamii
kuyapitia kwa makini masuala yote muhimu yanayojadiliwa kiundani kwa lengo la
kuyaelewa na pia kuyapatia ufumbuzi. Hatua hizi zinafahamika kama U3 (U Tatu)
ambapo ni:
Upimaji
(Utambuzi/Uibuaji) -------------------- Uchambuzi------------ Utekelezaji
Lengo
la uraghbishi huwa linatimia vema pale ambapo mambo yaliyoibuliwa yanaweza
kuchukuliwa hatua. Wakati wa uraghbishi wanajamii wataweza kufahamu masuala
kadhaa, kisha kuyachambua lakin pia watataka kucukua hatua kukabiliana na hali
kadhaa. Hii ni muhimu kwa sababu inazingatia uwezo wa jamii kuleta mabadiliko
na maendeleo badala ya kusubiri kufanyiwa kila kitu.
Upimaji: Hali ikoje?
Uchambuzi. Mambo gani yanasababisha hali hii?
Utekelezaji: Hatua zinazochukuliwa kwa misingi ya upimaji na uchambuzi.
Upimaji
Mbinu za kuibua: Jambo la
kwanza kwa mraghbishi ni kujua wanajamii wako wapi kimtazamo na kiufahamu. Hali
yao ikoje, maisha wanayaonaje? kwanini wanafanya wanavyofanya, ndoto zao ni
zipi, je ndoto zao zinatimilizwa na maisha wanayoishi sasa? Zinakwamishwa na
nini? Katika kuibua tunaweza pia kujua mtazamo ya wanajamii na uelewa wao
kuhusu masuala husika. Hivyo ni bora kutumia mbinu shirikishi zinazoibua na
wakati huohuo kuongeza uchambuzi.
Uchambuzi
Hatua ya pili ni kuchambua yale yote yaliyojitokeza katika hatu ya
kwanza. Hata tunahitaji kujua zaidi kuhusu hali na masuala husika. Mathalani
mara nyingi tunapata sababu zilizo wazi, kwa mfabo tunaweza kuambiwa sababu ya
wasichana wadogo kupata mimba kwenye jamii inatokana na ‘tamaa’ ama mkundi rika
yanayopotosha. Lakini waraghbishi hatukomei hapo. Tunataka kuuliza zaidi na
kuwaongoza wanajamii kuchambua sababu hizi za wazi ili kupata sababu za ndani
na za kina, na ia kuchambua sababu za kimfumo. Vivyo hivyo, bila kuwa na dhana
ya uchambuzi kijinsia inawezekana masuala ya jinsia hayataonekana.
Utekelezaji
Katika hali ya kawaida, kila mtu anatambua tatizo, analichambua kisha
anachukua hatua. Utekelezaji utafanyika kulingana na upimaji na uchambuzi
sahihi. Kuendeleza duara hili la u- tatu. Baada ya kuchukua hatua, inabidi
kutambua au kupima na kuchambua tena kama hatua zilizochukuliwa zimetatua
tatizo, au kubadili tatizo au kushindwa kabisa kukabili tatizo lenyewe.
Hata hivyo, ili U- Tatu
ifanikiwe, lazima kila hatua ichukuliwe kwa usahihi.
Lakini hii ni duara kwa sababu baada ya kuchukua hatua, inabidi kupima na
kuchambua matokeo ya hatua ili kuweza kuchukua hatua nyingine tena.
SEHEMU YA PILI.
Hatua muhimu za uraghbishi:
Mraghibishi anatakiwa kufuata hatua zifuatazo wakati anapoanza kutekeleza
majukumu yake ya kiuraghibishi.
Hatua pia zinahusisha mbinu anazotakiwa kutumia anapokuwa katika jamii.
Kujitambulisha
Mraghibishi anatakiwa kujitambulisha kwa uongozi wa jamii kabla hata ya
kuanza kazi na makundi ambayo yatashiriki katika uraghbishi. Hatua muhimu
inahusu kuripoti katika ofisi ya Halmashauri, kisha ofisi ya Kata ama ofisi ya
kijiji husika na kukutana na viongozi akiwemo Mtendaji kata/kijiji, mwenyekiti
wa kijiji/kitongoji ama ni muhimu kukutana na viongozi wote wa serikali ya kijiji.
Mraghbishi anajitambulisha na kuelezea kuhusu malengo ya shughuli yake na
namna atakavyofanya kazi katika jamii.
Ni vema kuwaomba wenyeviti wa serikali za mitaa/vitongoji kukupatia
makundi ya watu watakaoshiriki katika katika kazi ya uraghbishi. Kwa kuwa
inaweza kuwa vigumu kuita mkutano mmoja wa kikijiji na watu wote. Mraghibishi
anaweza kuomba ruhusa ya kupita mitaani/kijiji akiambatana na mwenyeji ambaye
ni kiongozi wa eneo hilo. Huko ataweza kuwaomba wale walio tayari ili kukaa
pamoja naye katika kikundi chenye watu kati ya
sita na kumi na mbili.
Ni vema kuendelea kuwaomba wale walio tayari kukutana nao siku inayofuata
ikiwa hamkuweza kumaliza mazoezi yote ya uraghbishi katika siku ya kwanza.
Ugawaji wa makundi
§
Vijana wa kike – miaka 15 – 24
§
Vijana wa kiume – miaka 15 – 24
§
Wanawake watu wazima
§
Wanaume watu wazima
§
Watu wenye ulemavu
§
Viongozi wa serikali ya kijiji
Unaweza kupanga makundi
kulingana na mahitaji ya uraghbishi, kwa mfano:
§
Vijana wa kike – miaka 13 – 17
§
Vijana wa kiume – miaka 13 – 17
§
Vijana wa kike – miaka 18 – 24
§
Vijana wa kiume – miaka 18 – 24
Baada ya kuwapata waeleze madhumuni ya mazoezi ya uraghbishi mnayokwenda
kuyafanya na hakikisha wanaelewa dhamira yako na jinsi wao watakavyonufaika na
masuala yatakayoibuliwa.
Kila kikundi kitafanya mazoezi kama yalivyoainishwa kulingana na
utaratibu wao. Kwa mfano kuna mazoezi maalum kwa kikundi cha vijana na mazoezi
maalum kwa vikundi vya watu wazima. Japokuwa makundi haya yanaweza kutumia
mbinu zote lakini ni muhimu kuangalia muktadha na utayari wa makundi hayo kabla
ya kujaribu ama kutumia mbinu hizi.
Kabla
ya kuanza waombe wanajamii kupanga muda gani ni mzuri kwao kwa ajili ya kufanya
kazi hii. Wekeni makubaliano kuhusu muda na jinsi mtakavyoifanya. Waambie
kwamba ‘hili ni zoezi la hiyari kwa ajili
ya maendeleo ya jamii yao, hivyo kila mmoja ana nafasi ya kuamua kama atapenda
kushiriki au lah’
Baada ya kupitia mazoezi yote kwa pamoja. Waambie kwamba watahitajika kwa
ajili ya kufanya mrejesho katika kikao kitakachohusisha viongozi wa kijamii.
Katika kila kundi mraghbishi awaongoze wanakikundi kuchagua kiongozi wao.
Kiongozi atakabidhiwa fimbo kama ishara ya kuwaongoza wengine na si kuwatawala.
Kwa kuwa yeye ndiye amekubalika miongoni mwa wengine, atakuwa na jukumu la
kuhakikisha kuwa mjadala unafuata taratibu na kila mmoja anapata nafasi ya
kuchangia. Haitakuwa tena kazi ya mraghbishi kuwaamsha wanajamii wachangie bali
anatakiwa kuwa na jicho la kuona nani anaweza kuchangia huku akiwasiliana na
kiongozi.
MBINU ZA URAGHBISHI. UPIMAJI.
Zoezi la kwanza: NANI MWENYE
NGUVU (Power Walk)
Zoezi hili litumike kwanza ili kutambua watu wenye uwezo ama wenye nguvu
na uhusiano wao na makundi mbalimbali katika jamii na kuchambua kwa nini
wengine wako mbele na wengine wanabaki nyuma. HATUA hii ni muhimu katika kuibua
mambo ya msingi kama ya kuanza kuyachambua. Zoezi hili linaweza kuwa na mantiki
zaidi iwapo wanajamii kwa pamoja wakiwemo viongozi wao pia wanaweza kushiriki
ili kutambua hali halisi ya jamii yao. Wachache kulingana na namna mraghbishi
atakavyopanga wanaweza kushiriki moja kwa moja na wengine wakibaki kwa ajili ya
mjadala.
Hatua za mraghbishi:
·
Tafuta eneo la wazi lenye nafasi ya kutosha kwa watu
kupiga hatua mbele angalao hatua ishirini.
·
Mgawie kila mwanajamii karatasi yenye mhusika mmoja.
·
Wahusika wawe mchanganyiko wa watu wenye uwezo,
viongozi wa kijamii, watu wenye ushawishi na hata wananchi wa kawaida (diwani,
mtendaji kata/kijiji, mwalimu mkuu, mfanyabiashara wa mazao n.k.) na wale wasio
na uwezo (mtoto yatima wa kike na kiume, mfanyakazi wa baa, kijana wa kijiweni,
msichana wa kazi wa mtendaji, msichana mwenye mtoto, n.k.) na wengine wa uwezo
wa kati.
·
Wapange katika mstari mmoja wakitazame mbele mahali uliposimama.
·
Kisha waambie kwamba utasoma kauli moja baada ya
nyingine. Kama jibu la mhusika ni ndiyo atapiga hatua moja kwenda mbele. Kama
ni hapana na haimhusu basi atabaki palepale.
·
Zoezi litaendelea namna hiyo mpaka masuala yote ambayo
yameandaliwa na mraghibishi yawe yameshasomwa yote.
·
Baada ya kumaliza kusoma na wakati tayari watu kadhaa
watakuwa wamepiga, anza kuwauliza wale walio mbele wajitaje wao ni wakina nani.
·
Wahoji mmoja mmoja kulingana na uwakilishi wao.
Wageukie walio nyuma na kuwaomba nao waeleze ni wakina nani.
Unaweza kutumia maswali haya kiujumla.
·
Kwa wale waliopo mbele,
mlijisikiaje wakati mnapiga hatua zaidi ya wengine?
·
Je mlifurahi kuona wengine
wakiwakaribia? Kwanini?
·
Kuna wakati wowote uligeuka
nyuma kuwatazama wengine? Ulijisikiaje?
·
Kwa
waliobaki nyuma; ulijisikiaje ulipoona wengine wanasonga mbele na wewe unazidi
kuachwa?
·
Hali hii inalingana vipi na
maisha halisi ya kijiji/kitongoji ama jamii
yenu?
·
Nani anaachwa nyuma? Kwanini?
·
Ikiwa hali hii inatokea,
tunaweza kuizungumziaje?
Mifano ya wahusika:
·
Mtendaji kata.
·
Mtendaji wa kijiji.
·
Mwenyekiti wa kijiji.
·
Mwalimu mkuu.
·
Daktari wa zahanati ya kijiji.
·
Mgambo wa kijiji.
·
Mfanyabiashara wa mazao.
·
Bibi mlezi wa yatima.
·
Msichana yatima umri wa miaka 14.
·
Mvulana yatima umri wa miaka 17.
·
Msichana mfanyakazi wa baa.
·
Mtoto wa Mtendaji kata.
·
Kijana wa kijiweni.
·
Mkulima mwanaume
·
Mama mjane mwenye watoto 6.
·
Mfanyabashara wa madini.
·
Mfugaji ndugu wa mbunge.
·
Kijana dereva wa bodaboda.
·
Mganga wa jadi.
·
Kibarua wa mashambani.
Mifano ya kauli
·
Nina umri wa zaidi ya miaka 30.
·
Napata angalao milo mitatu kwa siku.
·
Ninaweza kupata mkopo.
·
Sijawahi na sio rahisi kunyanyaswa kijinsia.
·
Naweza kumudu gharama katika hospitali
binafsi.
·
Sina haja ya kutafuta maji.
·
Ninaweza kwenda sekondari au nimekwenda sekondari.
·
Nina mradi wa uchumi.
·
Wakija wageni maarufu kijiji napata nafasi ya kukutana nao.
·
Ninaongea kwenye mikutano ya kijiji.
·
Nashiriki katika vikao vya bajeti ya
kijiji.
·
Nina uwezo wa kulipa ada ya shule.
·
Nina uwezo wa kumiliki radio na kupata taarifa mbalimbali.
·
Ninaweza kukutana na mbunge kila ninapohitaji.
Katika mjadala
unaweza pia kuibua masuala ya kiraghbishi mliyolenga kuyatazama, mathalani
masuala kuhusu mila, desturi kwa kuangalia ni nani kati ya wahusika mliowaona
ambao wana nguvu na ushawishi. Vilevile inaweza kuwa masuala kuhusu maji,
rasilimali, jinsia na hata ukatili wa kijinsia.
Zoezi la pili: UCHORAJI WA RAMANI
Baada ya kumaliza zoezi la kwanza la kuchambua watu wenye nguvu na namna
utofauti wake unavyoathiri mahusiano katika jamii, mraghbishi ataanza kukaa na
wanajamii kwa ajili ya zoezi la kutambua hali halisi ya jamii, kuhusu masuala
yanayohitaji kufanyiwa uraghbishi mathalani mila na desturi zinazochochea
ukatili kijinsia na nafasi ya mwanamke katika jamii. Uchoraji wa ramani pia
utatoa mwanga mzuri wa kujua jamii ianzie wapi katika kutafuta suluhu ya matatizo
yao na pia itakuwa ni chanzo cha kuweza kukusanya taarifa ndani ya kijiji na
kuzitafutia ufumbuzi kwa kushirikiana. Katika ramani wanajamii wataweza
kuainisha ni mazingira gani yanasababisha ama kuchochea vitendo vya ukatili
kijinsia, wapi matukio haya yanatokea, nani anahusika na pia ni aina gani ya
vitendo vya ukatili vinavyofahamika kwa wanajamii halikadhalika mila na desturi zilizopo.
Vilevile uchoraji wa ramani unawezesha kutambua mifumo mbalimbali ya
kijamii inayoweza kutumika kushughulikia masuala ya mila na ukatili wa
kijinsia. Wanajamii wanatakiwa kuchora ramani kwa kuonyesha mifumo na
miundombinu muhimu kama majengo ya serikali, ya kijamii, nyumba za ibada, kituo
cha polisi, ofisi ya asasi isiyo ya kiserikali nk.
Hatua za mraghbishi:
·
Tafuta eneo lenye kufaa kwa ajili ya kuchora ramani ya kijiji.
·
Wanaweza kuchora ramani chini kwenye udongo iwapo
hakuna karatasi kubwa na kalamu kwa ajili ya kufanya hivyo.
·
Waambie wanajamii wachore ramani ya kijiji/kitongoji
chao kwa kuonyesha mipaka ya kijiji na maeneo muhimu kama vile, barabara ‘kuu’,
ofisi za serikali ya kijiji, shule, zahanati, soko, mto, kituo cha polisi nk.
·
Pia waonyeshe mahali ambapo vijana wanakutana ama
hupenda kushinda kwa kuyawekea alama maeneo hayo. Wanaweza kutumia alama fulani
kuonyesha mahali ambapo vijana hukutana; alama kama vile jani ama kokwa ya
tunda nk.
·
Vilevile waonyeshe ni mahali gani ambapo mikutano ya
kijiji ama mikutano kwa ajili ya kufanya maamuzi huwa inafanyika. Wakati wa
kuonyesha waseme pia iwapo vijana wanahudhuria katika maeneo hayo ama
wanashiriki vipi?
·
Wataonyesha pia mahali na huduma tofauti za kijamii zinapopatikana.
Mraghbishi
anaweza kutumia maswali haya kuchokoza zaidi.
·
Kwa upande wa maeneo hatarishi:
o
Je ni maeneo gani ya hatari
zaidi katika jamii?
o
Ni hatari zipi zinapatikana
maeneo hayo?
o
Nani yupo
kwenye hatari zaii katika maeneo hayo? Wanawake? Wanaume? Vijana wa kike/kiume?
o
Nani anasababisha hatari hizo?
·
Kwa upande wa
huduma:
o
Ni huduma gani zinapatikana
katika jamii?
o
Wanawake wanapata huduma zipi?
o
Vijana wa kike na wa kiume
wanapata huduma hizi?
o
Nani anatoa huduma na kwa
kiwango gani? Km. afya, elimu, ulinzi, ushiriki nk.
·
Kwa upande wa
ulinzi:
o
Kuna mifumo
gani katika jamii ambayo inamhakikishia mwanamke, msichana ama kijana/wanaume
ulinzi dhidi ya ukatili kijinsia?
o
Nani anasimamia mifumo hiyo?
Kwa kiasi gani?
o
Mifumo inaaminika? Kwa
kiwango gani?
o
Changamoto
zipi zinapatikana katika masuala ya ulinzi dhidi ya vitendo vya ukatili
kijinsia?
·
Kwa upande wa utawala bora:
o
Wanasemaje kuhusu
uwajibikaji wa viongozi?
o
Wanaheshimu mawazo ya wananchi?
o
Kuna uwazi? Kwa kiasi gani?
o
Kuna njia gani za
kuwawajibisha viongozi wanapokiuka misingi ya utawala bora?
o
Njia hizo zinafanya kazi?
Kwa kiasi gani?
Tanbihi:
Si lazima mraghbishi afanye yote bali kwa yale muhimu ambayo yanahitajika
kwa kutegemea muktadha. Mazoezi hayapaswi kuwa marefu sana kiasi cha kuchukua
muda na kuwachosha wanajamii. Vinginevyo kama kuna mjadala mkali basi
mraghbishi anaweza kuendelea kwa dakika kadhaa. Muda mzuri zaidi kwa kila zoezi
ni dakika arobaini ama saa moja.
Zoezi la tatu: MSTARI WA KALENDA (Timeline).
Hii ni mbinu kwa ajili ya kuibua kutoka katika kundi la watu wazima. Mraghbishi ahakikishe kuwa anapata kundi
la watu wazima ambao wameishi katika jamii ama kijiji husika kwa muda wa
kutosha kuelewa kiundani ‘historia’ ya mahali hapo. Bila shaka watakuwa
wameshuhudia mabadiliko mengi katika mifumo ya maisha, uhusiano, mila na
tamaduni za mahali hapo.
Lengo ni kuwachokoza ili waweze kuorodhesha hali halisi ya jamii yao kwa
sasa kulinganisha na zamani. Mwishoni wataweza kuona ni wapi mambo yalibadilika
na sababu za mabadiliko hayo.
Hatua za mraghbishi:
·
Waulize wanajamii ni kwa muda gani wameishi katika eneo/kijiji ama
jamii hii.
·
Wanaweza kutoa mifano mmoja mmoja na utagundua kuwa
pengine idadi kubwa wameishi mahali hapa kwa zaidi ya miaka 20 ama 30 nk.
·
Sasa waambie kwamba utataka kujua historia ya mahali
hapa katika masuala yanayohusu uhusiano wao katika jamii na hapa mtaibua namna
mila na desturi zilivyobadilika ama kutekelezwa.
·
Waambie kwamba hamtaweza kuangalia kila kitu kuhusu
historia bali mambo fulani machache ili nawe ujifunze kutoka katika masimulizi
yao.
·
Sasa waombe wachore mstari mmoja mnyoofu chini ya
ardhi. Wataanza na kuweka tarehe (mwaka) ya mwanzo wanayotaka kuanza nayo km.
1973 mwanzo wa mstari. Kisha wataanza kuorodhesha matukio kadhaa yaliyojitokeza
tangu wakati huo hadi kufikia sasa.
(matukio yawe yanayohusu namna uhusiano
katika jamii ulivyobadilika, matukio gani yaliathiri mila na desturi zao nk)
·
Wahimize waendelee kuchora na kukukumbuka, kwa mfano ‘Vita ya Kagera’, ‘Kipindi
ambacho jamii yao ilikubwa na ukame, njaa, magonjwa, vifo nk na kwamba haya
yote yalibadili vipi desturi zao na kuathiri mila zao kwa namna gani.’
Baada ya kumaliza unaweza
kupitia mstari wao na kuuliza maswali:
·
Mabadiliko haya yaliathiri
vipi uhusiano kati ya wanajamii?
·
Kulikuwa na
mila ama taratibu gani za kumlinda mwanamke ama kijana dhidi ya ukatili wa
kijinsia?
·
Ni mila zipi zilitelekezwa?
Nani alizitelekeza? Kwanini?
·
Je ni vijana ama wazee ndio
walioacha mila hizi?
·
Ni wakati gani vitendo vya
ukatili kijinsia vilionekana kushamiri? Kwanini?
·
Kulikuwa na utaratibu gani
wa kushughulikia masuala ya ukatili kijinsia?
UCHAMBUZI:
Hatua ya pili baada ya UPIMAJI (uibuaji) ni UCHAMBUZI. Hapa mraghibishi
atawaongoza wanajamii kuweza kuchambua na kujua sababu za kina kwa masuala
ambayo yaliibuliwa katika hatua iliyopita ili kupata kiini cha jambo na kuweza
kulishughulikia.
Zoezi la kwanza: UPANGAJI
WA VIPAUMBELE 1 (Ranking)
Kupiga kura.
Zoezi hili
linaweza kutumika kama zoezi la mwanzo la kujenga msingi kwa ajili ya kupata
mambo ya muhimu kabisa. Itampa nafasi kila mwanajamii kupiga kura na kutaja
jambo moja ambalo yeye anaamini kuwa ndilo la msingi zaidi linalohitaji
kushughulikiwa kutokana na athari zake kwa jamii. Baada ya kuwa wanajamii wote
wameorodhesha mambo yaliyotokana na sehemu ya kwanza ya uraghbishi, wakumbushe
kuwa mtaanza kufanya tathmini ya kila mmoja. Itakuwa rahisi kwao kuyataja kwa
sababu watakuwa wameshaanza kuyaibua kwenye mstari wa kalenda, na uchoraji wa ramani.
Hapa wanajamii
watapiga kura ili kupata jambo moja la mwisho kwa kila mmoja ambalo ndilo
litawekwa katika orodha ya upangaji mawe. Inategemewa kwamba kwa kuwa mawazo ya
wanajamii yatatofautiana basi yale ambayo yamebaki kwa kila mmoja yatajumuishwa
kati hatua inayofuata.
Hatua za mraghbishi:
·
Waambie wanajamii wafikiria kuhusu mila na desturi
ambazo wanazifahamu na ambazo hutekelezwa mara kwa mara katika jamii.
·
Kisha wagawie kila mmoja vikaratasi vitano.
·
Kila mmoja aandike aina tano za mila na desturi katika
vipande vidogo vya karatasi (ikiwa wote wanaweza kuandika). Ama wanaweza
kutumia vijiti na alama tofauti.
·
Baada ya kila mmoja kuwa na vikaratasi vitano ambapo
kila kimoja kimeandikwa aina ya ukatili kijinsia, sasa waambie kuwa watapaswa
kufanya maamuzi magumu.
·
Waambie kuwa kila mmoja ajifikirie kwamba yupo ndani
ya mtumbwi na anasafiri majini akiwa na masuala hayo matano anayotaka kuyashughulikia.
·
Lakini kwa kuwa hali ya bahari imechafuka, analazimika
kuondoa baadhi ya mizigo na kuitosa baharini ili kupunguza uzito wa chombo.
Hapo utamtaka kila mmoja kuondoa karatasi moja yenye aina mojawapo ya mila na
desturi ambayo anahisi haina athari sana kulinganisha na nyingine.
·
Endelea kuwaambia wapunguze karatasi moja kila mara na
kubaki na zile ambazo wanaona ni lazima kufika nazo pwani ili ziweze
kushughulikiwa. Wataendelea kupunguza
mpaka pale watakapobaki na karatasi moja tu. Hii itamaanisha kuwa kila mmoja
amebaki na suala moja ama aina moja ya mila na desturi ambayo inamkera zaidi.
·
Watake kila mmoja asome ya kwake na kisha ziandike.
·
Pitia orodha pamoja na wafahamishe kwamba haya ndio
masuala ama aina za mila ambazo zina umuhimu sana kushughulikiwa. Km kurithi wajane, ukeketaji, utakasaji wa
wajane wanapofiwa na waume zao, jando na unyago yenye mafunzo yasiyofaa kwa
watoto, marufuku kutojadili masuala ya ukatili kijinsia, nk.
·
Yachukue masuala hayo kwa ajili ya zoezi linalofuata.
Zoezi la pili: UPANGAJI WA VIPAUMBELE 2
Upangaji wa
mawe.
Hii ni mbinu inayotumika kwa ajili ya kuchagua mambo ambayo yana athari
zaidi ya mengine katika jamii husika kutokana na mitazamo wa wanajamii. Orodha
hiyo ya vitendo vya ukatili kijinsia itaweza kutokana na zoezi lililopita.
Ikiwa masuala ni mengi mnaweza kupiga kura na kupata masuala matano ama sita tu
ambayo itakuwa rahisi kuyapitia.
Hatua za mraghbishi:
·
Kwa kushirikiana na wanajamii, anza kutaja masuala
yote yaliyoorodheshwa kutoka katika hatua ya kwanza ya uibuaji.
·
Waonyeshe jinsi ya kupanga mawe. Angalia
mfano hapa chini
·
Baada ya kupata orodha, waambie kwamba sasa watapiga
kura ili kujua athari za kila jambo na kuangalia ni nani anaathirika zaidi.
·
Wakusanye mawe madogo
ishirini kwa ajili ya kuyapanga. Kisha wachore jedwali
na
kuweka chumba cha kwanza ‘masuala’, halafu ‘wanaume’ na mwisho ‘wanawake’
·
Waorodheshe masuala yote kisha waanze kugawa mawe kwa
kutoa idadi kubwa kwa yale yaliyo na uzito zaidi. Kama wanaona suala la kurithi
wajane linahitaji uzito zaidi wanaweza kuweka mawe matano au sita, kisha kama
suala la ukeketaji linafuata wanaweka mawe matatu au manne na kuzidi kufanya
hivyo kwa kila jambo.
·
Waambie kwamba wanaruhusiwa kubadilisha ikiwa wamefika mwisho na hawaridhiki.
Mfano wa jedwali
Masuala |
Wanawake |
Wanaume |
kurithi wajane |
5 |
3 |
marufuku kutojadili
masuala ya ukatili kijinsia |
2 |
5 |
jando na unyago yenye mafunzo yasiyofaa kwa watoto |
3 |
6 |
utakasaji wa wajane
wanapofiwa na waume zao |
4 |
3 |
ukeketaji |
6 |
3 |
|
|
|
|
|
|
Angalizo: Epuka kumpa kila
mwanajamii mawe kadhaa ili apige kura kwenye jambo analoona ni muhimu sana.
Japo kwa kufanya hivi kazi itaisha haraka lakini hakutakuwa na mjadala. Wakati
wa kupanga mawe wanajamii wanatakiwa kujadili, kubishana na kukubaliana. Wakati
wanafanya hivi watatoa hoja ambazo ndizo msingi wa zoezi.
Hapa hoja nyingi
zitaibuka na mraghbishi ataweza kuendelea kuchokoza na kuandika yatokanayo na
mjadala.
Zoezi la tatu: MADUARA YA UCHAMBUZI (Venn Diagram).
Zoezi hili
linalenga katika kuchambua namna masuala mbalimbali mathalani ya mila, desturi,
ukatili kijinsia yanavyomuathiri hususani mwanamke. Mraghbishi atawachoza
wanajamii ili waweze kujadili na kueleza ni nani anayeathiriwa zaidi na mila na
desturi zilizotajwa. Katika makundi yatakayotajwa inaweza kujitokezwa kwamba
wanawake ana vijana hasa wasichana ndio waathirika zaidi wa mila na desturi
zinazotajwa. Mraghbishi ataandaa kadi za duara zenye ukubwa tofauti kulingana
na orodha ya masuala ama mila na desturi zilizoorodheshwa.
Hatua za mraghbishi:
§ Waulize
wanajamii ni mila na desturi zipi zinazotekelezwa kwa kiasi kikubwa. Kisha ile
ambao inatekelezwa kwa kiasi kikubwa itapewa duara kubwa na kuandikwa humo. Hii
itafuatiwa na mila ama desturi ambayo haitekelezwi sana kwa kupewa duara ndogo
mpaka kufikia ile ndogo zaidi kwa mila na desturi ambazo hazitokei mara kwa mara.
§ Waambie washiriki wazunguke
wakisimama kwenye duara.
§ Mwombe
kiongozi aweke duara moja ndogo ambayo inamwakilisha mwanamke/mwanajamii katikati.
§ Kisha mpe
mwanajamii yeyote katika kundi aweke kadi mojawapo jirani na ilipo kadi ya
mwanamke. Anaweza kuweka kadi hii karibu kabisa ama mbali zaidi.
§ Bila kujali
ukubwa wa kadi, kwa kadiri inavyokuwa karibu inamaanisha kwamba jambo hilo lina
athari kubwa zaidi.
§ Na kwa
kadiri kadi inavyokuwa mbali inamaanisha jambo hilo halina athari sana. Kwa
mfano, kurithi wajane si mila inayotekelezwa kwa kiasi kikubwa hivyo ni kadi
ndogo lakini inapotokea athari zake huwa ni kubwa sana. Kwa vyovyote kadi hii
italetwa karibu zaidi na ilipo kadi inayomwakilisha mwanamke/mwanajamii.
§ Waruhusu
wanajamii wapange kadi huku wakijadili sababu za wao kufanya hivyo, wakibishana
na kueleza zaidi mpaka watakaporidhika.
UTEKELEZAJI.
Sehemu hii inahusu mbinu mbalimbali za kutumia kwa ajili ya kuweka
mikakati kuhusu yale ambayo tayari makundi yamepitia. Utekelezaji utafanyika
katika mkutano wa mrejesho ambapo makundi yote yatakutana pamoja na uongozi wa
kijiji.
Mara baada ya mazoezi ya uraghbishi kwa kila kikundi, panga kuhusu
mkutano wa mrejesho kwenye ngazi ya kijiji. Kila kikundi kitajiandaa kufanya
mrejesho wa yale waliyoyajadili, kuyaibua
na kuyachambua. Ikiwa washiriki ni wengi basi kila kikundi kitachagua
wawakilishi wawili wa kuhudhuria mrejesho wa kijiji.
Zoezi la kwanza: NDOTO ZETU
Baada ya kila kikundi kufanya mrejesho wake, waraghbishi wataandika yale
yote ambayo yameonekana kupewa kipaumbele. Hapa lazima kuangalia ni masuala
gani ambayo yanajirudia kutoka katika vikundi vyote.
Kwa kutegemea na muda na nafasi, inaweza kufanyika kwa kutumia makundi
manne ambapo viongozi wa kijamii wanaweza kuchanganyika katika vikundi vya
wanaume au kama ni viongozi wanawake katika kikundi cha wanawake na pia vijana
wa kiume na wa kike.
Hatua za mraghibishi:
·
Waombe wanajamii wachore mstari mrefu unaojulikana kama ‘mstari wa maisha’.
Wanaweza kuugawa mstari huo
katika sehemu tatu kuanzia wakati walipo sasa.
·
Sehemu ya kwanza
·
Sasa mpaka miaka mitano ijayo
·
Sehemu ya pili:
·
Miaka mitano hadi kumi
·
Sehemu ya tatu
·
Miaka kumi hadi kumi na tano/ishirini
·
Katika kila sehemu waambie wanajamii wawe huru kuchora
ndoto zao kwa kuzingatia masuala yale yaliyoibuliwa katika mijadala ya vikundi
na katika mrejesho.
o
Ni jamii ipi wanayoitaka
katika kipindi fulani cha maisha?
Wanaweza kutafuta
kauli mbiu wakati wa
kuchora, km. ‘Jamii yetu bila mila kandamizi.’
o
Mabadiliko gani
wanayotarajia kuyaona?
o
Aina gani
ya mahusiano ambayo wangependa kuyaona baina ya wanawake, wanaume, vijana wa
kiume na wa kike pamoja na watoto.
o
Mifumo gani
ya ulinzi dhidi ya ukatili wa kijinsia kwa kuangalia
mila na desturi zinazoweza kuongeza ulinzi.
·
Wanafanya hivi kwa kuchora lakini wasisitize kwamba
uchoraji wao uwe na uhalisia kulingana na hali na matarajio ya jamii yao.
·
Mwishoni fanya mjadala ili kujua
o
Wanatarajia kufanya nini ili kutimiza ndoto zao?
o
Nani anaweza kufanya nini?
o
Mkakati gani wanajiwekea?
Zoezi la pili: UCHAMBUZI WA
MAJUKUMU
Baada ya kuchora ndoto zote, waraghibishi wataandika kile ambacho jamii
inatarajia. Hapa pia wasisahau kuhusu masuala yaliyoibuka katika mrejesho kama
sehemu ya mambo muhimu yanayotakiwa kutekelezwa.
Hatua za mraghbishi:
Waambie wanajamii kuwa wanatakiwa kuorodhesha watu wote waliopo kwenye
jamii kulingana na vyeo na majukumu yao, kwa
mfano:
·
Mwenyekiti wa kijiji.
·
Mtendaji.
·
Mwenyekiti wa ulinzi na usalama.
·
Diwani.
·
Wazee wa mila.
·
Ngariba.
·
Muuguzi
·
Nyakanga/kungwi.
·
Mzee maarufu
·
Mtaalamu wa afya.
·
Asasi inayofanya kazi kijijini nk.
Wanajamii watachora jedwali lifuatalo na kuweka kila mmoja na nafasi
yake. Kwanza wataandika jina/cheo cha mhusika katika sehemu ya jedwali
inayoonyesha mhusika, halafu wataangalia kuhusu ndoto zilizopo na masuala
yaliyopendekezwa kufanyika na kisha watasema kuhusu nini anapaswa kufanya ili
kufikia ndoto hiyo. Katika sehemu moja wanaweza kuwa watu zaidi ya mmoja.
Mwishoni watatoa alama kulingana na uwezo wake. Kwa mfano namba 1 itamaanisha
uwezo mdogo na namba 10 itamaanisha uwezo mkubwa kabisa.
Angalia mfano
Mhusika |
Suala/ndoto husika |
Wajibu wake
kufikia ndoto |
Uwezo wake |
Mtendaji |
Kuunda
kamati ya ulinzi na usalama |
Kuweka
mipango ya wananchi |
10 |
|
|
Kuitisha
mkutano wa kijiji kujadili masuala ya
ukatili wa kijinsia |
|
Mwenyekiti wa ulinzi na usalama |
Kukomesha vitendo vya ukatili |
Kurudisha
ulinzi shirikishi Kuhakikisha
kuwa kamati ya ulinzi |
10 |
|
|
inafuatilia
matukio yote ya ukatili na
kuyaripoti |
|
Mzee wa mila |
Kuondoa mila zote kandamizi |
Kuitisha kikao cha wanamila, mangariba na makungwi
ili kuajdili
mila kandamizi nk. |
8 |
Baada ya kufanya hivi, makundi yatapitia na kukubaliana kwa pamoja. Ikiwa
muda hautoshi waraghibishi watapitia na kuweka majumuisho pamoja na kisha
kurudisha nakala kwa uongozi wa kijiji kwa ajili ya utekelezaji.
Wakati wa
mkutano wa mrejesho kijijini, wanajamii watachagua timu ya wawakilishi kwa
ajili ya mrejesho kwnye ngazi ya halmashauri. Wawakilishi watapata nafasi ya
kukaa na waraghbishi na kuandaa mrejesho wo kwa kuangalia masuala wanayotaka
kuongea na viongozi wa serikali ambayo yanahitaji kushughulikiwa na pia
wanaeleza kuhusu hatua wanazopanga kuchukua.
Wakati wa
mrejesho wa Halmashauri, waraghbishi (wanajamii) wataomba kukutana na
Mkurugenzi wa Halmashauri pamoja na wakuu wa idara husika.
No comments:
Post a Comment