Ushiriki Katika Kilimo
Sera ya
Maendeleo ya Wanawake na Jinsia (2000) iliweka mkazo katika kuongeza ushiriki
wa wanawake katika kilimo ambacho ni uti wa mgongo na njia ya kujikimu kimaisha
kwa wananchi wengi hususan wanaoishi vijijini. Jitihada mbalimbali zimefanyika
katika kuboresha sekta ya kilimo ikiwa ni pamoja na: Kuunganisha kilimo na
usalama wa chakula na lishe ili kukabiliana na tatizo la lishe duni kwa
kuzingatia programu ya Lishe na Usalama wa Chakula; na utekelezaji wa Mkakati
wa Taifa wa Lishe; Utekelezaji wa programu ya Feed the Future, Bread
Basket Initiative; Programu ya Kuboresha Miundombinu ya Masoko na Kuongeza
Thamani na Asasi ya Huduma Ndogo za Kifedha Vijijini (Rural Finance Support
Program); Kuboresha Maisha ya wafugaji kupitia programu ya Maendeleo ya
Sekta ya Mifugo (2008) na kuandaa Sera ya Masoko ya Bidhaa za Kilimo (Agricultural
Marketing Policy). Jitihada nyingine ni pamoja na uanzishwaji wa programu
zifuatazo: Ukanda wa Ukuaji wa Kilimo Kusini mwa Tanzania - SAGCOT; MKUKUTA
Iⅈ Kilimo Kwanza; Mradi Shirikishi na Uwezeshaji wa Maendeleo ya Kilimo
- PADEP; na DADIP ambazo zimeimarisha huduma za ugani kwa wakulima kupitia
mashamba darasa na vituo vya kata vya maarifa na taarifa za kilimo; Kuongeza
idadi ya zana za kilimo kwa wakulima wadogo mfano trekta za mikono (power
tillers); na Kuwajengea uwezo wakulima, Asasi za Wakulima, Sekta Binafsi, watoa
huduma na Maafisa Ugani.
Sekta ya
kilimo bado inakabiliwa na changamoto licha ya juhudi kubwa za serikali na
wadau. Changamoto hizo ni pamoja na athari za mabadiliko ya tabianchi,
uzalishaji mdogo kutokana na matumizi ya teknolojia duni za kilimo, ujuzi mdogo
kwa wakulima na ukosefu wa masoko na taarifa za masoko. Kutokana na kutokuwepo
kwa usawa wa kijinsia, wanawake tofauti na wanaume, wana fursa finyu ya kupata
mikopo na ujuzi. Hali hii inasababisha wanawake washindwe kuajiri na kuwekeza
kwenye kilimo cha mazao yenye thamani kubwa. Aidha, uwezo wa wanawake kumiliki
rasilimali za uzalishaji kama vile ardhi ni mdogo. Hivyo, wanawake wakulima
humiliki wastani wa ukubwa wa shamba la asilimia 40 tu ambayo inazalisha mazao
kidogo. Matokeo ya utafiti wa Sensa ya Kilimo iliyofanyika 2019/20 yanaonesha
kuwa kati ya kaya 12,007,839 Tanzania, kaya 7,837,405 (65.3%) zinajihusisha na
shughuli za kilimo. Kwa upande wa Tanzania bara, kati ya kaya 7,657,185 (65.7%)
zinazojihusisha na kilimo, kaya 4,972,372 (64.9%) zinalima mazao, kaya 2,526,846
(33%) mazao na ufugaji na kaya 157,290 (2%) zinajishughulisha na ufugaji pekee.
Serikali ina
jukumu la kushirikiana na wadau kuhamasisha masuala ya kijinsia katika sekta ya
kilimo ili kuhakikisha kuwa wanawake na wanaume wanapata haki sawa. Uboreshaji
wa miundombinu ya kilimo vijijini (barabara, miundombinu ya umwagiliaji na
mifumo ya TEHAMA) unapaswa kuimarishwa ili kuongeza tija kwa wakulima wa
vijijini na kuboresha usalama wa chakula na lishe. Upatikanaji wa huduma za
kifedha (mikopo na ujuzi wa usimamizi wa kifedha) kwa wakulima wanawake wa
vijijini ni lazima ziboreshwe ili kutoa fursa zaidi za kupanua uwekezaji wao wa
kilimo ili kuongeza kipato zaidi.
No comments:
Post a Comment