Jinsia na Haki za Binadamu
Mfumo wa sheria wa Tanzania una jukumu muhimu katika
kuhakikisha kwamba kuna utekelezwaji kamili wa haki za binadamu na kwamba kila
raia anafurahia haki zake bila kuingiliwa. Serikali ya Tanzania imejitolea
kukuza na kulinda haki za binadamu kwa kutekeleza mipango mbalimbali ya ndani na
kimataifa. Ndani ya nchi Serikali imejitahidi kuwajengea uwezo maafisa wa
mahakama kuhusiana na sheria za kimataifa za haki za binadamu, ikiwa ni pamoja
na haki za wanawake, katika muktadha wa CEDAW, itifaki yake ya hiari na Itifaki
ya Mkataba wa Afrika wa Haki za Binadamu na Watu na Haki ya Wanawake barani
Afrika. Katika mwaka wa 2011, majaji 24 na wasajili wa Mahakama Kuu walipata
mafunzo katika vyombo vya kimataifa vya haki za binadamu, hasa vinavyohusu wanawake
na watoto. Vile vile, Serikali ilihakikisha kuwa haki za binadamu zinafundishwa
katika shule zote za msingi na sekondari (kama mada katika uraia) na pia katika
Vyuo vya Elimu ya Juu (HLIs), ikilenga kuwajengea kizazi kipya hisia ya
kuheshimu haki za binadamu.
Serikali pia
imeimarisha vifungu vya sheria kwa vitendo vya ubaguzi, ambavyo vinanyima haki
za vikundi vingi vya kijamii kulingana na usawa wa kijinsia. Mifumo ya kisheria
iliyoanzishwa imegawanyika katika sekta zote, na hivyo kufanya haki za binadamu
kuwa suala mtambuka. Sheria hizi ni pamoja
na; Sheria ya Mtoto ya mwaka 2009;
Sheria ya Kuzuia na Kudhibiti UKIMWI (Na. 28 ya mwaka 2008); Sheria ya Taifa ya
Uchaguzi ya mwaka 1985 ambayo inakataza ubaguzi katika chaguzi; Sheria ya
Masharti Maalum ya Makosa ya Kujamiiana (SOSPA) ya mwaka 1998 pia imejumuishwa katika Kanuni ya
Adhabu; Sheria ya Ardhi ya mwaka 1999, na Sheria ya Msaada wa Kisheria ya mwaka
2017. Mifumo hiyo kwa ujumla inasaidia ustawi wa wanawake kiuchumi na kijamii;
inatoa ulinzi wa wanawake na watoto dhidi ya unyanyasaji wa kijinsia katika
mazingira mbalimbali; inajenga thamani na kuhakikisha wanawake wana haki ya
kupata, kumiliki na kutumia ardhi kwa usawa na wanaume.
Hata hivyo,
maendeleo yaliyopatikana, mianya ya kisheria na desturi za kimila mara nyingi
hudhoofisha haki za wanawake. Wasichana bado wanaolewa chini ya umri wa miaka
18 na kama matokeo ya kuenea kwa mifumo ya sheria za kimila. Ripoti ya UNICEF
(2016), inathibitisha kuwa kiwango cha ndoa za utotoni ni zaidi ya mara mbili
ya wastani wa dunia wa asilimia 13. Takriban
asilimia 30 ya wasichana wenye umri wa miaka 15-19 ama wameolewa, wametalikiwa
, wajane au wapo katika ndoa za kitamaduni na hawawezi kujihusisha na shughuli
za uzalishaji mali. Vikwazo vingine ni pamoja na kushindwa kutekeleza likizo ya
uzazi iliyoongezwa na muda wa kunyonyesha katika uchumi usio rasmi na sekta
binafsi, pamoja na kuenea kwa vitendo vya ukatili wa kijinsia katika jamii
nyingi nchini kote.
Serikali inapaswa
kujitahidi kuimarisha ushirikiano wa sekta mbalimbali na ushirikishwaji wa sekta
binafsi katika jitihada za kuboresha ulinzi wa haki za binadamu nchini kote.
Jitihada pia zinapaswa kuwekwa katika: kurekebisha Sheria ya Ndoa Na.5 (1971)
na sheria nyingine zinazohusiana na urithi, mirathi na haki za watoto pamoja na
sheria nyingine za kibaguzi; kutoa mafunzo ya uhamasishaji wa Sheria
zinazozingatia masuala ya kijinsia kwa maafisa wa utekelezaji wa sheria,
wataalamu wa huduma za sheria na wadau wengine; na maandalizi ya nyenzo za
mafunzo na kampeni kuhusu haki za kisheria za wanawake na kuzisambaza ipasavyo.

No comments:
Post a Comment