Monday, February 6, 2023

TEN/MET yawasilisha mapendekezo ya bajeti yenye mrengo wa Kijinsia Bungeni

 

Na Deogratius Temba

Mtandao wa Elimu Tanzania (TEN/MET) umewasilisha mapendekezo ya Bajeti yenye mrengo wa Kijinsia kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge, jijini Dodoma.


Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti wakiwa katika picha ya pamoja na wanachama wa Mtandao wa Elimu Tanzania baada ya kuwasilisha mapendekezo ya Bajeti yenye mrengo wa Kijinsia.Mwenye suti nyeusi mbele kabisa ni Mwenyekiti wa Kamati  Mhe. Daniel Sillo.


Mapendekezo hayo ambayo yanalenga kuishawishi serikali kuingiza masuala ya Kijinsia kwenye sekta ya Elimu ili kuongeza ubora wa elimu unaowanufaisha wanafunzi wa kike, kiume na wenye ulemavu yamewasilishwa kwa kwmaati ya Kudumu ya Bunge wakati ambapo mchakato wa bajeti kwa mwaka wa fedha 2023/2024 unaendelea.

Miongoni mwa mapendekezo yaliyowasilishwa kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ni pamoja na:

Utengwaji wa bajeti kwa ajili ya kutoa pedi bure kwa wanafunzi; ambapo TEN/MET ilishauri kwamba serikali iondoe  kodi ya VAT kwenye bidhaa za hedhi salama.  Na pia serikali itenge fedha kwenye Bajeti zake za elimu kwa ajili ya kuwezesha wasichana kupatiwa taulo za kike bure shuleni.

Kutokana na kuendelea kuwepo kwa mdondoko wa wanafunzi wa kike na wa kiume kwenye mfumo wa elimu ya msingi na sekondari.  TEN/MET ilipendekeza, kuweka mkazo kwenye ujenzi wa mabweni katika shule za kata na kuhakikisha watoto wanapata chakula shuleni

Pia TEN/MET ilipendekeza kwamba  serikali iangalie namba ya kuongeza bajeti ya  Miundombinu mfano idadi toshelezi ya vyoo vyenye mfumo wa maji tiririka kwenye shule za msingi na sekondari. “Tunapendekeza, bajeti kwaajili ya SWASH program isimamiwe kikamilifu kuondoa changamoto hii. Halmashauri ambazo hazipo kwenye miradi ya SWASH zielekezwe kutenga fedha kupitia mapato ya ndani ili vyoo vinavyojengwa viweze kuwa na miundombinu yenye kukidhi mahitaji ya hedhi salama, hii itasaidia wasichana wanaoingia hedhi kushiriki masomo kwa siku zote bila kukosa” alisema sehemu ya mapendekezo hayo iliyowasilishwa na Deogratius Temba, mchambuzi na mkufunzi wa Bajeti yenye mrengo wa Kijinsia.

Pia ilielezwa  kwamba wasichana walio acha masomo kwa  ujauzito wanakumbana na changamoto mbalimbali wakati wa kurejea shuleni katika mfumo rasmi na usio rasmi.   Na kupendekeza kwamba serikali imarishe vituo vya kutolea elimu ili viwe rafiki kwa wanafunzi hao

Awali akitoa utangulizi kwa mbele ya  Kamati, Meneja Programu wa TEN/MET, Bi. Martha Makala, alisema kwamba TEN/MET ni Mtandao mpana unaoundwa na mashirika Zaidi ya 180 ambayo yanafanya kazi nchi nzima yakiwa ynajishughulisha na afua mbalimbali za elimu hasa utetezi kwenye usawa wa Kijinsia katika elimu.

Alisema kwamba, pamoja na kufanya afua za kutoa elimu, mashirika wanachama wa TEN/MET waliosambaa kila kona ya nchi wamechangia kwa kiasi kikubwa ujenzi wa miundombinu ya kutolea elimu chini kwa kushirikiana na halmashauri za wilaya.

No comments:

Post a Comment