Friday, June 7, 2024

TGNP na UNFPA wawezesha jamii kuibua vitendo vya Ukatili wa Kijinsia Kasulu

 TGNP na UNFPA wawezesha jamii  kuibua vitendo vya Ukatili wa Kijinsia  Kasulu


Washiriki katika hafla ya kutoa mrejesho wa Utafiti Shirikishi (Participatory Action Research) kutoka kata za Kumsenga na Murusi, Halmashauri ya Mji wa Kasulu, Kigoma, Utafiti huo umewezeshwa na TGNP na UNFPA ili kutokomeza Vitendo vya Ukatili wa Kijinsia 



Na Deogratius Koyanga, Kasulu

Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP)  wamefanya mrejesho wa Utafiti raghibishi (Participatory Action Research [PAR]) uliofanyika katika kata ya Mrusi na Kumesenga, Halmasahuri ya Kasulu Mji.

Utafiri shirikishi huo ni sehemu ya mradi wa kutokomeza vitendo vya Ukatili wa Kijinsia unaotekelezwa na TGNP na Shirikla la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia idadi ya watu (UNFPA), unaotekelezwa katika wilaya ya Kasulu chini ya program ya Pamoja ya Mashirika ya Umoja wa Kimataifa

Katika wasilisho lao, washiriki wa PAR katika Halimashauri ya Kasulu Mji, walisema kwamba kupitia mchakato wa PAR uliowezeshwa na TGNP kwa kutumia mbinu za U-3 za Uibuaji, Uchambuzi na Utekelezaji, wameweza kuibua sababu za kina za kushamiri kwa vitendo vya Ukatili wa Kijinsia kwa wanawake na watoto katika eneo hilo na kubaini njia za utatuzi wake ambazo kwa kushirikiana na viongozi wa ngazi za serikali za mitaa na wilaya watashirkiana na kuhakikisha vinakoma.

“Tumeona jinsi ambavyo kata zetu hizo, mbili zimeadhirika na vitendo vya ubakaii, ulawiti na mimba za utotoni, hatutaki hali hii iendelee, tutahakikisha sasa kwa kushirkiana na viongozi wetu tunazuia kabisa kwa kushirikiana na viongozi wetu.”alisema Beatrice Christopha msomaji wa risala mbele ya Mkurugenzi wa Halmashauri.

“Tumejifunza pia kuwahusisha viongozi wetu kama madiwani na watendaji wote wa serikali tulio nao katika ngazi ya mitaa, kata na wilaya ili kupata ufumbuzi wa changamoto zilizo nje ya uwezo wetu sisi kama wananchi. Katika mchakato huu wa siku sita, tulijadili kwa kina, tulichambua kwa kina na tuliweza kuibua changamoto mbalimbali ndani ya Kata zetu” alisema  Beatrice

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, Mabena Paschalina, alisema kwamba kazi iliyofanywa na TGNP ni kubwa kuwajengea uwezo wananchi hao uwezo na kujitambua na kuamua kuchukua hatua za changamoto za kukidhiri kwa vitendo vya ukatili wa Kijinsia.

“Nyie mliojengewa uwezo na TGNP ni wazazi lakini pia mnaishi miongoni mwa jamii, ambako vitendo vya Ukatili vinatokea, ninawataka sasa tuchukue hatua, tupite kwenye mikutano, vikao, majukwaa, kwenye taasisi za dini, shuleni nk. Kuhakikisha ujumbe unawafikia watu wazima lakini pia na watoto” alisema

Kaimu Mkurugenzi amesema kwamba, Halmasahuri itaendelea kutoa ushirkiano kwa wadau kama TGNP na UNFPA katika kutekeleza afua za usawa wa Kijinsia, sambamba na kuhakikisha kwamba jamii inabadilika kimtazamo na kitabia kwa kusimamia vizuri sheria, kanuni na taratibu za nchi ili kuwepo na haki na usawa.

Ameongeza kwamba, halmashauri kwa kushirikiana na vyombo vingine, itahakikisha  kwamba wananchi wote wanakuwa salama, hawafanyiwi vitendo vya Ukatili wa Kijinsia ili waweze kunufaika na fursa zilizopo na uwekezaji mkubwa unaofanywa na serikali ya Tanzania kuwezesha wananchi kiuchumi. 

Kikao hicho cha mrejesho kilihudhuriwa pia na wakuu wa idara na Vitengo wa Halmasahuri pamoja na Mkuu wa dawati la Jinsia -Polisi Kasulu, ambao walipata nafasi ya kujibu baadhi ya masuala yaliyoibuliwa ambayo yapo chini ya maeneo yao ya kiutendaji.

wengine waliohudhuria ni watendaji kata mbili za Kumsenga na Murusi, Madiwani wa kata  na viti maalum na Maafisa Maendeleo ya jamii wa kata husika.
















No comments:

Post a Comment