Wajibu wa Mzazi au mlezi kulinda haki za Mtoto Kisheri
Na Mwandishi wetu
Tumeshuhudia matukio mengi katika jamii yetu ya watoto
kunyanyaswa na kudhalilishwa na watu wazima wakiwemo walezi na hata baadhi ya
wazazi wasio waadilifu.
Imekuwa kawaida kusikia watoto yatima au wanaolelewa na watu
wa karibu kama sana wakitendewa vitendo
vya uonevu baada ya wazazi wao kufariki. Ndugu na jamaa, bila haya, wamekuwa
wakifanya maamuzi yanayowahusu watoto bila kuzingatia maslahi na haki za
watoto.
Unyanyasaji wanaofanyiwa watoto, wakati mwingine unafanyika
kwa sababu wazazi, walezi na hata jamii kwa ujumla hawafahamu wajibu walionao
kwa mtoto kisheria. Kutokujua namna mtoto anavyolindwa kisheria kunaweza, kwa
namna moja au nyingine, kuchochea vitendo hivi.
Katika [blogu] hii kila Alhamisi, tunakusudia kukuletea
dondoo muhimu kama zinavyoainishwa kwenye sheria ya Mtoto Na. 21 ya 2009
iliyotungwa kwa minajili ya kulinda maslahi na ustawi wa mtoto.
Sheria hii ilitungwa na serikali yetu kukidhi matakwa ya
mikataba ya kimataifa inayomhakikishia mtoto haki zake za msingi. Lakini pia
sheria na. 21, inatekelezwa sambamba na sheria Sheria ya kanuni za adhabu sura ya 16 (SOSPA 1998), Sheria ya ndoa ya
mwaka 1971, Sheria ya Mtoto ya mwaka 2009 na Sheria ya Elimu ya Elimu ya mwaka
1978. Kwahiyo watu wasifikiri kwamba watapona endapo sheria zitasimamiwa
vizuri. Kuna vifungu na adhabu za kutosha kwa mtu anayefanya Ukatili wa
Kijinsia kwa watoto.
Kwa mhutasari, sheria na. 21 ya mwaka 2009, yaani sheria ya
mtoto hii inalenga kumwekea mtoto
mazingira ya kukua na kustawi katika nyanja zote za kimaisha bila
kudhalilishwa, kuonewa na kunyanywaswa na jamii ikiwemo familia yake. Ingawa
msisitizo ni kumlinda mtoto zaidi, sheria hii pia inafafanua wajibu wa mtoto kwa
familia na jamii kwa ujumla.
Labda tuanze na tafsiri ya mtoto. Mara nyingi tumetumia neno
‘mtoto’ kumaanisha mambo mengi kwa wakati mmoja. Kwa mfano, unaweza kushangaa mzee
wa miaka 55 anajitambulisha kama ‘mtoto’ wa tatu katika familia yake. ‘Mtoto’
huyu wa tatu, naye anaweza kuwa na ‘watoto’ kadhaa wenye umri wa utu uzima.
Hapa mtoto maana yake ni nini? Mtoto, katika mazingira hayo,
ni mtu aliyezaliwa na mtu mwingine bila kujali umri wake. Tafsiri hii
inazingatia uhusiano wa mzazi na mwanae bila kujali umri.
Kadhalika, unaweza kusikia mtu mwenye miaka 40 akidaiwa
kufanya mambo ya kitoto. Utoto, kwa mazingira hayo, ni kufanya vitendo
visivyoakisi uwezo wa mtu mzima anayejitegemea. Jamii inakuwa na matarajio
fulani kwa mtu anayejitambulisha kama mtu mzima. Anatarajiwa kufikiri kwa namna
fulani, kufanya vitu kwa namna fulani na hata kuonekana kwa namna fulani.
Mchoro huu unao onyesha Ukatili wa watoto ni kwahisani ya TGNP
Inapotokea mtu mzima huyu anashindwa kukidhi matarajio hayo, watu humtazama kwa jicho la ‘utoto.’ Utoto ni sifa mbaya kwa mtu mzima.
Lakini, kidini tunaambiwa ‘msipokuwa kama watoto wadogo
hamuwezi kuurithi uzima wa milele.’ Mtoto, katika mukhtadha huu, si sifa mbaya.
Tabia za kitoto kimsingi ni sharti muhimu la kumpa mtu sifa za kuuona ufalme wa
mbinguni.
Hata hivyo 'mtoto' huyu anaelekezwa kuendelea kukua na
kuongezeka ili awe na sifa ya kujitegemea na kuwategemeza wengine. Haifai
kuendelea kuwa 'kama watoto wachanga' wanaoendelea kuwategemea wengine. Jambo
hili linaelezwa kisaikolojia pia.
Kisaikolojia mtoto anaweza kuwa mtu yeyote bila kujali umri
wake ambaye bado anaendelea kukua kiakili, kimwili, kiroho na kimahusiano. Hata
hivyo, mtu mwenye miaka pungufu ya 12 ana nafasi kubwa ya kuwa na sifa hizi.
Sababu kubwa ni kuwa katika umri huo, mtu huyu bado
anaendelea kukomaa na kupevuka kiakili, kimwili, kiroho na kimahusiano. Ndio
kusema mtu ambaye bado hawezi kujitegemea kimwili, kiakili, kiroho na kijamii,
ana sifa za kuitwa mtoto.
Kwa kuwa tafsiri za ‘mtoto’ na ‘utoto’ zinaweza kuwa na
mkanganyiko mkubwa kama tulivyouona hapo juu, sheria hii imetumia kigezo kimoja
cha umri kumtambua mtu mwenye sifa za kuitwa mtoto.
Mtoto, kwa mujibu wa sheria hii, ni mtu yeyote mwenye umri
wa chini ya miaka 18. Haijalishi amepevuka akili kiasi gani, maadam ana umri
usiozidi miaka 18 mtu huyo bado ataendelea kutambuliwa na sheria hii kama
mtoto. Yapo mashirika yanayofanya kazi ya usaidizi kwa vitendo vya Ukatili
ambayo baadhi ni: TWALA, WILDAF, WILAC, TAMWA,
CRC, KIWOHEDE, Maafisa Ustawi wa Jamii wa Halmashauri zote, Maafisa maendeleo
ya jamii wa halmashauri zote ambao pia wapo kwenye ngazi ya Kata. Kamati za
Ulinzi wa mama na mtoto za Wilaya, Kata na Vijiji, Viongozi wa Dini. Zaidi pia
simu bure namba. 116.
No comments:
Post a Comment