Wednesday, September 7, 2022

Wajibu wa Mzazi au mlezi kulinda haki za Mtoto Kisheria

 

Wajibu wa Mzazi au mlezi kulinda haki za  Mtoto Kisheri

Na Mwandishi wetu

Tumeshuhudia matukio mengi katika jamii yetu ya watoto kunyanyaswa na kudhalilishwa na watu wazima wakiwemo walezi na hata baadhi ya wazazi wasio waadilifu.

Imekuwa kawaida kusikia watoto yatima au wanaolelewa na watu wa karibu kama sana  wakitendewa vitendo vya uonevu baada ya wazazi wao kufariki. Ndugu na jamaa, bila haya, wamekuwa wakifanya maamuzi yanayowahusu watoto bila kuzingatia maslahi na haki za watoto.

Unyanyasaji wanaofanyiwa watoto, wakati mwingine unafanyika kwa sababu wazazi, walezi na hata jamii kwa ujumla hawafahamu wajibu walionao kwa mtoto kisheria. Kutokujua namna mtoto anavyolindwa kisheria kunaweza, kwa namna moja au nyingine, kuchochea vitendo hivi.

Katika [blogu] hii kila Alhamisi, tunakusudia kukuletea dondoo muhimu kama zinavyoainishwa kwenye sheria ya Mtoto Na. 21 ya 2009 iliyotungwa kwa minajili ya kulinda maslahi na ustawi wa mtoto.

Sheria hii ilitungwa na serikali yetu kukidhi matakwa ya mikataba ya kimataifa inayomhakikishia mtoto haki zake za msingi. Lakini pia sheria na. 21, inatekelezwa sambamba na sheria Sheria ya kanuni za adhabu  sura ya 16 (SOSPA 1998), Sheria ya ndoa ya mwaka 1971, Sheria ya Mtoto ya mwaka 2009 na Sheria ya Elimu ya Elimu ya mwaka 1978. Kwahiyo watu wasifikiri kwamba watapona endapo sheria zitasimamiwa vizuri. Kuna vifungu na adhabu za kutosha kwa mtu anayefanya Ukatili wa Kijinsia kwa watoto.

Kwa mhutasari, sheria na. 21 ya mwaka 2009, yaani sheria ya mtoto  hii inalenga kumwekea mtoto mazingira ya kukua na kustawi katika nyanja zote za kimaisha bila kudhalilishwa, kuonewa na kunyanywaswa na jamii ikiwemo familia yake. Ingawa msisitizo ni kumlinda mtoto zaidi, sheria hii pia inafafanua wajibu wa mtoto kwa familia na jamii kwa ujumla.

Labda tuanze na tafsiri ya mtoto. Mara nyingi tumetumia neno ‘mtoto’ kumaanisha mambo mengi kwa wakati mmoja. Kwa mfano, unaweza kushangaa mzee wa miaka 55 anajitambulisha kama ‘mtoto’ wa tatu katika familia yake. ‘Mtoto’ huyu wa tatu, naye anaweza kuwa na ‘watoto’ kadhaa wenye umri wa utu uzima.

Hapa mtoto maana yake ni nini? Mtoto, katika mazingira hayo, ni mtu aliyezaliwa na mtu mwingine bila kujali umri wake. Tafsiri hii inazingatia uhusiano wa mzazi na mwanae bila kujali umri.

Kadhalika, unaweza kusikia mtu mwenye miaka 40 akidaiwa kufanya mambo ya kitoto. Utoto, kwa mazingira hayo, ni kufanya vitendo visivyoakisi uwezo wa mtu mzima anayejitegemea. Jamii inakuwa na matarajio fulani kwa mtu anayejitambulisha kama mtu mzima. Anatarajiwa kufikiri kwa namna fulani, kufanya vitu kwa namna fulani na hata kuonekana kwa namna fulani.

  Mchoro huu unao onyesha Ukatili wa watoto ni kwahisani ya TGNP 

Inapotokea mtu mzima huyu anashindwa kukidhi matarajio hayo, watu humtazama kwa jicho la ‘utoto.’ Utoto ni sifa mbaya kwa mtu mzima.

Lakini, kidini tunaambiwa ‘msipokuwa kama watoto wadogo hamuwezi kuurithi uzima wa milele.’ Mtoto, katika mukhtadha huu, si sifa mbaya. Tabia za kitoto kimsingi ni sharti muhimu la kumpa mtu sifa za kuuona ufalme wa mbinguni.

Hata hivyo 'mtoto' huyu anaelekezwa kuendelea kukua na kuongezeka ili awe na sifa ya kujitegemea na kuwategemeza wengine. Haifai kuendelea kuwa 'kama watoto wachanga' wanaoendelea kuwategemea wengine. Jambo hili linaelezwa kisaikolojia pia.

Kisaikolojia mtoto anaweza kuwa mtu yeyote bila kujali umri wake ambaye bado anaendelea kukua kiakili, kimwili, kiroho na kimahusiano. Hata hivyo, mtu mwenye miaka pungufu ya 12 ana nafasi kubwa ya kuwa na sifa hizi.

Sababu kubwa ni kuwa katika umri huo, mtu huyu bado anaendelea kukomaa na kupevuka kiakili, kimwili, kiroho na kimahusiano. Ndio kusema mtu ambaye bado hawezi kujitegemea kimwili, kiakili, kiroho na kijamii, ana sifa za kuitwa mtoto.

Kwa kuwa tafsiri za ‘mtoto’ na ‘utoto’ zinaweza kuwa na mkanganyiko mkubwa kama tulivyouona hapo juu, sheria hii imetumia kigezo kimoja cha umri kumtambua mtu mwenye sifa za kuitwa mtoto.

Mtoto, kwa mujibu wa sheria hii, ni mtu yeyote mwenye umri wa chini ya miaka 18. Haijalishi amepevuka akili kiasi gani, maadam ana umri usiozidi miaka 18 mtu huyo bado ataendelea kutambuliwa na sheria hii kama mtoto. Yapo mashirika yanayofanya kazi ya usaidizi kwa vitendo vya Ukatili ambayo baadhi ni: TWALA, WILDAF, WILAC, TAMWA, CRC, KIWOHEDE, Maafisa Ustawi wa Jamii wa Halmashauri zote, Maafisa maendeleo ya jamii wa halmashauri zote ambao pia wapo kwenye ngazi ya Kata. Kamati za Ulinzi wa mama na mtoto za Wilaya, Kata na Vijiji, Viongozi wa Dini. Zaidi pia simu bure namba. 116.

No comments:

Post a Comment