Hali ya Upatikanaji na Umiliki wa
Ardhi kwa wanawake
Sera ya Maendeleo ya Wanawake na
Jinsia (2000) ilitoa kipaumbele katika eneo la upatikanaji, umiliki na utumiaji
wa ardhi kwa usawa baina ya wanawake na wanaume. Umiliki na utumiaji wa ardhi
ni nguzo muhimu katika suala zima la maendeleo ya wanawake kiuchumi.
Hivyo, umiliki wa ardhi kwa wanawake ni muhimu
katika kufikia fursa nyingine za kiuchumi nchini. nchini Tanzania, ni wanawake
26% wanamiliki ardhi ya kilimo (SIGI, 2020). Hali hii inatokana na kuendelea
kuwepo kwa mila na desturi zinazowapendelea wanaume kurithi na kumiliki ardhi
ya familia ambapo wanawake hupata fursa hiyo kupitia wanaume ndani ya familia.
Serikali imeendelea na jitihada
za kisera ili kuhakikisha kuwa umiliki wa ardhi unazingatia usawa wa kijinsia.
Sera hizo ni pamoja na Sera ya Taifa ya Maendeleo ya Makazi (2000), Sera ya
Taifa ya Ardhi (1995), Ibara mbalimbali za Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania (1977) na Dira ya Maendeleo 2025. Jitihada nyingine ni pamoja na
Marekebisho ya Sheria ya Ardhi ya Vijiji Na. 5 ya mwaka 1999 kifungu cha 3 (2)
ambayo inatoa fursa kwa kila mwanamke kumiliki na kutumia ardhi na kuanzisha
Kamati za kuhamasisha haki za wanawake kumiliki ardhi mwaka 2017. Kutokana na
jitihada hizi, mwaka 2018 jumla ya hati 80,000 za umiliki wa ardhi
zilisajiliwa.
Jitihada hizi zimewezesha
kuongezeka kwa idadi ya wanawake wanaomiliki ardhi kutoka asilimia 9 hadi
asilimia 25 na kuongezeka kwa umiliki wa pamoja kutoka asilimia 6 hadi asilimia
16; kuongezeka kwa watu wenye hati miliki zinazotambulika kisheria kutoka
asilimia 50 mwaka 2016 hadi asilimia 59 mwaka 2018; kuongezeka kwa idadi ya
hati za kimila za umiliki wa ardhi mfano, katika Mkoa wa Iringa pekee jumla ya
hati za kimila 3,208 zilitolewa (1,970 Wilaya ya Kilolo na 1,238 Wilaya ya
Mufindi). Hii ni matokeo ya uwezeshaji wa Shirika Lisilo la Kiserikali la Haki
Ardhi linalohamasisha uandaaji wa mipango ya matumizi bora ya ardhi katika
vijiji 7 katika Wilaya ya Mufindi na 11 katika Wilaya ya Kilolo.
Pamoja na mafanikio
yaliyopatikana, suala ya umiliki wa ardhi na rasilimali nyingine za uzalishaji
limeendelea kuathiri maendeleo ya wanawake ambapo licha ya kuwa na sheria
zinazowalinda wanawake katika kumiliki rasilimali bado mila na desturi kandamizi
ni kikwazo. Umiliki wa rasilimali za kiuchumi kwa wanawake kama vile pato la
familia, ardhi, vitendea kazi na mikopo umeendelea kuwa mdogo ukilinganisha na
wanaume. Pamoja na ukweli kwamba wanawake wanachangia Katika sekta ya kilimo
uvuvi na misitu, wanawake wamachangia asilimia takribani asilimia 67 (ILFS,
2014).
Kiwango cha uzalishaji kwa
wanawake katika sekta ya kilimo ni kidogo ikilinganishwa na wanaume. Hii ni
kutokana na matumizi ya zana duni kama vile jembe la mkono. Sheria ya Mirathi
ya Kimila (1963) inazuia wanawake, wajane na wasichana kurithi ardhi na hivyo
kuwakosesha fursa za kumiliki rasilimali za kiuchumi na uwekezaji. Hivyo,
maboresho katika sheria ni muhimu katika kuwawezesha wanawake kuboresha hali
zao za kiuchumi na kijamii. Kwa msingi huo, ni muhimu kuiwezesha jamii
kushiriki na kuwa na uelewa wa haki za wanawake kurithi mali ikiwemo ardhi.
No comments:
Post a Comment