Mambo ya kuzingatia kabla na wakati wa kuandika wosia
Hapo awali nilikuwa nikiamini kuacha
wosia ni uchuro yaani kujitakia au kujitabiria kifo chako mwenyewe. Hii
ilipelekea nikaogopa mnoo inapotokea nikisikia habari zinazohusu masuala ya
wosia. Hali kadhalika ninaamini pia wapo watu wengi wanaoogopa kuacha wosia kwa
dhana hii hii kwamba ni uchuro wa kujitabiria kifo.
Wengine nao huamini ya
kwamba wosia unaachwa na watu wasomi au wazee au wanaume au wanaokaribia kufa
au wenye uwezo mkubwa kwenye kumiliki mali kama vile nyumba, viwanja, hisa
kwenye makampuni au pesa katika akaunti za Benki na kadhalika.
Yote hayo yatajibiwa
na makala hii hatua kwa hatua ambapo nitaangazia kwa ufasaha ni nini maana ya
wosia kwa jicho la kisheria zaidi, aina zake, sifa, pamoja pia na faida.
Tutaweza pia kuangalia japo kwa uchache wosia unatakiwa uweje.
Nini basi maana ya wosia?
Wosia ni tamko lenye
nguvu kisheria ambapo mtoa wosia anakusudia ni namna gani mali yake au zake
zitasimamiwa baada ya kifo chake. Katika wosia mtoa wosia anaweza kuelezea ni
kwa namna gani mali yake au zake zitagawanywa kwa warithi wake, kiwango ambacho
watagawiwa, orodha ya mali anazomiliki, orodha ya wadai na wadaiwa, namna gani
atazikwa na kadhalika.
Hiyo ni baadhi
tu ya orodha ya mambo yanayotakiwa yawepo katika wosia na ni vyema kila jambo
ambalo ni muhimu kuandikwa katika wosia ili kuondoa utata. Ikumbukwe kuwa
mwacha wosia hatakuwa hai ili aweze kuulizwa kuhusiana na wosia wake wakati
utakapoanza kutumika hivyo basi ni vyema uandikwe kwa lugha iliyo wazi na yenye
kueleweka vizuri. Utata wowote utakaojitokeza unaweza kupelekea wosia
kubatilishwa na wosia huo utakuwa batili automatiki.
Ikumbukwe ya kuwa
kutokuacha wosia au kuacha wosia wenye dosari itapelekea mali utakazoacha
kugawanywa kwa utaratibu wa wasioacha wosia. Utaratibu huu unaweza ukawa sio
rafiki sana kwani wakati mwingine unaweza kwenda kinyume kabisa na matakwa ya
mtoa wosia.
Aina za wosia
Wosia wa mdomo
Huu ni wosia
unaotolewa kwa maneno ya mdomo yaani ‘Oral will’. Japokuwa aina hii ya wosia ni
ngumu wakati mwingine kuthibitishwa lakini sharia inautambua kuwa ni
wosia kama vile ulivyo ule wa maandishi. Kwa mfano, Local Customary Law
(Declaration) (No. 4) Order, 1963 inataka wosia huu ni lazima utolewe wakiwepo
mashahidi wanne (4) yaani wawili wawe ni ndugu na wawili wasiokuwa ndugu. Mke
au wake za marehemu, kama anaye au anao, ni lazima awe nyongeza ya
mashahidi hao. Kigezo hiki kisipofuatwa basi wosia huo utabatilishwa kweupee.
Wosia wa maandishi
Huu ni wosia
unaotolewa kwa njia ya maandishi. Wakati mwingine unajulikana kama wosia rasmi.
Lengo lake ni sawa tu kama lilivyo la wosia wa mdomo kama nilivyoeleza hapo
juu. Umakini wa hali ya juu sana unatakiwa uzingatiwe katika kuandika wosia
huu.
Ni lazima ‘legal
formality’ yaani matakwa ya kisheria yafuatwe wosia wa aina hii
unaopoandikwa. Baadhi ya matakwa hayo ni kama vile ni lazima uwe kwa maandishi
na kusainiwa na mtoa wosia huo mbele ya mashahidi, ushuhudiwe angalau na
mashahidi wawili na ni vizuri mmoja kati yao akawa ni nduguye mtoa wosia;
mashahidi hao wanaweza kuzidi wawili ila tu wasipungue.
Wosia wa maandishi
unaweza ukabatilisha wosia uliotolewa awali kwa mdomo, isipokuwa wosia wa mdomo
hauwezi kubatilisha ule wa maandishi. Na anayeweza kufanya hivyo ni mtoa
wosia peke yake na si mtu mwingine.
Wosia uliotolewa na watu wawili kwa lengo la pamoja
Huu unaitwa kwa lugha
ya kitaalamu ‘a mutual will’. Wosia huu unatolewa na watu wawili wenye malengo
ya pamoja kama nilivyodokeza hapo juu kwa maana ya kwamba wote wanakubaliana
jambo au mambo yanayofanana.
Wosia huu unapendelewa
sana na walio katika mahusiano ya kimapenzi kama vile wanandoa. Kwa mfano
kwenye wosia huu wanaweza wakakubaliana katika wosia huo ya kwamba yeyote
atakayetangulia kufariki kati yao basi mali zitaenda kwa yule aliyebakia hai,
kama vile mume akitangulia kufariki basi mali walizonazo zitamilikiwa na mke na
kinyume chake, halafu wanaweza pia kukubalia namna gani watoto wao watapata
urithi baada ya wote kufariki.
Hii ijulikane ya
kwamba makubaliano haya kama yalikwisha kuwekwa hakuna namna yanaweza
kubadilishwa kama mmoja wapo wa watoa wosia huo kashafariki.
Wosia wa masharti fulani
Unaweza ukauitwa
‘Conditional will’ ambapo masharti fulani aliyoyaweka mtoa wosia na ni lazima
yatimizwe kwanza ndipo tunaweza kusema wosia una nguvu kisheria. Msharti haya
yanatakiwa yawe ni yale yanayotekelezeka.
Kwa mfano mtoa wosia
anaweza kusema nyumba hii apewe Comfort pindi atakapooa au atakapoweza kupata
Shahada yake ya kwanza ya Sheria, hivyo basi ikiwa mtoa wosia huo amefariki
nyumba hiyo haitokwenda kwa Comfort mpaka atakapokuwa ameoa au kupata Shahada
yake ya kwanza ya Sheria.
Mambo ya msingi
yanayotakiwa kuzingatiwa wakati wa kuandaa wosia
Wosia ni lazima uwe na
mambo yafuatayo vinginevyo inaweza kupelekea ukabatilishwa na mpango wa
kugawanya mali bila wosia ukachukua nafasi. Mambo hayo ni kama vile:
1.
Mtoa wosia ni lazima
kisheria awe na uwezo wa kuacha wosia. Hapa nina maana ya kwamba sharia
inahitaji mtu anayetoa wosia awe na umri wa miaka isiyopungua kumi na minane
(18). Pia anatakiwa awe na akili timamu wakati wa kuacha wosia huo. Hali kadhalika
mtu mwenye matatizo ya akili anaweza kuandika wosia pindi tatizo hilo
limemwondoka kwa mfano endapo atakuwa anasumbuliwa na tatizo la ukichaa wa muda
‘temporary insanity’. Mtu akiwa na akili timamu na akaandika wosia lakini
baadae akapata ukichaa wosia ule hautokuwa batili kwani wakati anauandika
alikuwa na utimamu wa akili.
2.
Mtoa wosia ni lazima
afahamu yale yaliyoandikwa katika wosia. Kwa mfano mwacha wosia kaandikiwa
wosia eidha na wakili au mtu yeyote ni lazima afahamu yale yaliyoandikwa ndani
kabla hajaweka saini.
3.
Wosia ni lazima utaje
majina ya mtoa wosia.
4.
Wosia unatakiwa utaje
atakaye simamia mirathi.
5.
Wosia ni lazima uwe na
tarehe ya siku wosia huo ulipoandaliwa.
6.
Wosia ni lazima utaje
aina na kiwango cha thamani ya mali zinazotolewa katika wosia. Kama kuna kitu
kinamilikiwa na watu wawili au zaidi basi ni sharti hilo libainishwe katika
wosia.
7.
Wosia unatakiwa utaje
idadi ya warithi na wanufaika wa mirathi hiyo.
8.
Wosia unatakiwa utilie
maanani vipi itakapotokea mrithi au warithi na mnufaika au wanufaika watakapofariki
kabla ya mtoa wosia.
9.
Wosia unatakiwa utilie
maanani ndoa inayoweza kufungwa baada ya wosia kuandaliwa. Ndoa itakayofungwa
baada ya wosia kuandikwa inaweza kuathiri wosia huo.
10.
Wosia ni lazima
usainiwe na mtoa wosia mbele ya mashahidi.
11.
Wosia ni lazima
uthibitishwe na mashahidi.
12.
Mtoa wosia ni lazima
aonyeshe ya kuwa ameandika wosia huo akiwa na akili timama pia bila
kushurutishwa.
13.
Lazima katika wosia
kuwe na kipengele kinachoonyesha ya kuwa mtoa wosia akibatilisha wosia wowote
alioutoa awali.
14.
Endapo mtu ambaye kwa
kawaida alitakiwa kupewa sehemu ya mirathi lakini hakutajwa katika wosia basi
ni vyema sababu zikatolewa.
15.
Endapo mambo haya
yatazingatiwa itapunguza kwa kiasi kikubwa matatizo yanayoweza kutokea baadae
mtoa wosia atakapokuwa amekwisha fariki, mfano, wosia huo kukataliwa au
kubatilishwa kwa kutokufuata taratibu kama nilivyokwisha kuelezea kwa uchache
hapo awali.
Muhimu: Ifahamike ya kwamba hakuna fomula maalumu ya kuandika
wosia lakini endapo utazingatia mambo niliyoyataja hapo juu basi wosia wako
utakuwa una nguvu kama wosia mwingine wowote.
Faida za kuacha wosia
·
Humsaidia mtoa wosia
kupanga ni namna gani mali yake itakavyosimamiwa baada yakufariki kwake. Endapo
atafanya hivyo basi itamzuia mtu asiyehusika kuingilia mali zake pindi
atakapofariki.
·
Kuepuka mali alizoacha
kugawanywa kwa utaratibu wa asiyeacha wosia. Upoutaratibu ambapo mtu asiyeacha
wosia mali zake kugawanywa kinyume cha matakwa yake kama nilivyoeleza hapo
awali hivyo basi ili kuepusha jambo kama hili kutokea ni vyema kabisa
ukajiwekea utaratibu wako ambao utaheshimiwa na kila mtu.
·
Kuepusha watu
wadanganyifu wenye nia ya kutaka kunufaika na mali alizokuwa amechuma marehemu.
·
Wosia utamwezesha mtoa
wosia kumweka mtu mwaminifu atakayesimamia mali zake baada ya yeye kufariki.
Pia utamsaidia kuandaa walezi wa mtoto au watoto wake. Jaribu kufikiri mazingira
ambayo baba mwenye mtoto au watoto kafariki na pengine mkewe nae kafariki au
hawaishi wote na pengine mtoa wosia huyo ndugu zake wa kuzaliwa walimtangulia
auhana kabisa, katika mazingira haya marehemu asipoandaa utaratibu mzuri wa
kusimamia mirathi basi mali na watoto alioacha watakuwa katika mazingira magumu
sana. Wosia tu ndio utakaookoa hilo lisitokee.
·
Wosia utasaidia
kufahamu mali za marehemu na nani apewe nini na kipi.
·
Wosia pia utaweza
kueleza utaratibu wa namna mtoa wosia atakavyozikwa. Hapa ataweza kuelezea
azikweje, wapi na kwa gharama zipi kutoka wapi. Unaweza hata kuamua uchomwe
moto badala ya kufukiwa na waliobakia watahakikisha hilo linatokea.
Je ni wakati gani sahihi
kwa mtu kuandika wosia?
Lengo kuu la wosia ni
kutaka mambo fulani fulani yafanyike pindi mtu atakapokuwa umefariki.
Tusikariri ya kuwa ni lazima tuwe na vitu vingi ndio tuweze kuacha wosia kwani
unaweza hata kuacha wosia kuutoa mwili wako pindi utakapofariki utumike katika
kufanyia majaribio kwa wanafunzi wa udaktari katika chuo cha udaktari cha
Muhimbili.
Ukizingatia vigezo
vingine kama vile umri na kadhalika, mtu yeyote anaweza kuacha wosia. Hata kama
unayo mali yenye thamani ndogo bado ni muhimu kwa wewe kuacha wosia kama
nilivyoweza kuelezea hapo juu.
Unaweza ukaacha wosia
kwenye mambo mengine ukiacha mali na vitu kama nilivyokwisha kudokeza hapo juu.
Hivyo basi wosia unaweza kuachwa wakati wowote mtu anapokuwa hai na sio
kusubiria mtu yupo mahututi ndio anatoa wosia.
Ni nani anapaswa kuandika
wosia?
Mtu yeyote, awe
mwanaume au mwanamke, kijana au mzee, mwenye mali nyingi au chache, mwenye umri
wa miaka kumi na minane (18) na kuendelea akiwa na akili timamu wakati wa
kuacha wosia basi anakidhi vigezo vya kuacha wosia.
Muhimu
Ni muhimu pia kufahamu
ya kuwa wosia unakusudiwa kuwa na nguvu pale mtoa wosia huo atakapofariki. Watu
wafahamu wosia ni tamko au karatasi tu kama aliyeandika wosia huo bado yupo
hai. Itambulike pia mali zitakazopatikana baada ya wosia kuachwa zinaweza kuwa
sehemu ya wosia bila hata kuorodheshwa katika wosia huo.
Lakini pia wosia wa
mwanzo unaweza kufutwa au kubadilishwa na wosia mwingine. Hii inaweza kutokea
hata kama kuna kipengele katika wosia kinachosema wosia huo hautabadilishwa
kamwe. Jambo hili linaweza kufanywa na aliyetoa wosia kipindi cha uhai wake na
sio mtu mwingine yeyote.
Mwisho naendelea
kukusisitiza ndugu msomaji wangu usikose mwendelezo wa Makala hizi. Endelea
kuutembelea ukurasa huu ili kujipatia makala mbali mbali kuhusiana na sheria.
Kumbuka ‘learning is a process’ kwa maana ya kwamba kujifunza
ni mchakato hivyo usichoke kujifunza. MAKALA HII NI KWA MUJIBU WA: https://ijuesheriatz.wordpress.com/2017/09/04/mambo-ya-kuzingatia-kabla-na-wakati-wa-kuandika-wosia/
No comments:
Post a Comment