Thursday, April 3, 2025

Hedhi Salama: Muheza Yaendelea Kufanikiwa Baada ya Utekelezaji wa WASH

 

** Hedhi Salama: Muheza Yaendelea Kufanikiwa Baada ya Utekelezaji wa WASH**

Na Deogratius Koyanga

Upatikanaji wa huduma za hedhi salama umeleta mabadiliko makubwa kwa wasichana shuleni, ukirejesha tabasamu na kuwapa fursa ya kushiriki kikamilifu katika masomo yao.

Mwongozo wa serikali juu ya Maji, Afya na Usafi wa Mazingira wa mwaka 2016 unatoa maelekezo kwa wadau mbalimbali kuhakikisha ujenzi wa miundombinu ya hedhi salama mashuleni ili kuboresha mazingira ya kujifunzia kwa watoto wa kike. Kupitia mwongozo huu, kila Halmashauri inapaswa kutenga bajeti kila mwaka wa fedha ili kuhakikisha changamoto zinazotokana na ukosefu wa huduma bora za Maji, Afya na Usafi wa Mazingira (SWASH) zinatatuliwa na hivyo kuimarisha kiwango cha elimu.

Serikali ya Tanzania kupitia hotuba mbalimbali za viongozi wake imekuwa ikisisitiza umuhimu wa bajeti kwa ajili ya huduma za hedhi salama. Rais Samia Suluhu Hassan katika moja ya hotuba zake aliwahi kusema, "Tunahitaji kuhakikisha kuwa hakuna msichana anayekosa shule kwa sababu ya hedhi. Serikali itaendelea kuweka mkazo katika bajeti ya elimu na afya ili kuboresha mazingira ya watoto wa kike." Aliyekuwa Waziri wa Afya Ummy Mwalimu,  pia alisisitiza kuwa mpango wa bajeti ya taifa unahakikisha kuwa shule zinatengewa fedha za kuboresha miundombinu ya afya na usafi wa mazingira.

Katika utekelezaji wa mwongozo huu, Mtandao wa Jinsia (TGNP) kwa kushirikiana na Shirika la ONGAWA na Halmashauri ya Wilaya ya Muheza walitekeleza mradi wa Maji, Afya na Usafi wa Mazingira (WASH) mwaka 2022 katika ngazi ya kaya na shuleni, huku suala la hedhi salama likipewa kipaumbele ili kuwawezesha wasichana kuhudhuria masomo yao bila kikwazo. Ingawa mradi huo umekamilika, ufuatiliaji wa hivi karibuni umebaini mafanikio makubwa yanayoendelea kuwanufaisha wasichana na jamii kwa ujumla.

Utafiti wa awali wa serikali wa mwaka 2009 kuhusu hali ya SWASH ulionyesha kuwa hali ya Maji, Usafi wa Mazingira mashuleni ilikuwa duni, ambapo ni asilimia 11 tu ya shule zilizofanyiwa utafiti zilikuwa na uwiano wa matundu ya vyoo unaokidhi viwango vya kisera. Zaidi ya asilimia 20 ya shule zilikuwa na uwiano wa wanafunzi 100 au zaidi kwa tundu moja la choo, huku asilimia 6 ya shule zikiwa hazina kabisa matundu ya vyoo. Hali hii iliathiri mahudhurio ya wasichana shuleni, hususan wakiwa kwenye hedhi, kutokana na ukosefu wa vifaa vya hedhi salama na mazingira yasiyokuwa na faragha.

Katika Shule ya Sekondari ya Zirai, wilayani Muheza, wasichana wamepata unafuu mkubwa baada ya kujengewa chumba maalum cha kujisitiri wanapokuwa kwenye hedhi, kupatiwa pedi za bure shuleni, maji safi na salama kwenye vyoo, pamoja na elimu na malezi bora kutoka kwa walimu wa kike. Wasichana wanasema sasa wanaweza kuhudhuria masomo bila wasiwasi, tofauti na awali ambapo wengi walikuwa wakikosa vipindi wanapokuwa kwenye hedhi. Afisa Elimu Kata ya Zirai, Mwalimu Mohamed Mmole, anasema kuwa mafanikio haya yamechangiwa na uamuzi wa shule kutoa kipaumbele kwa hedhi salama. Hata kwa changamoto ya upatikanaji wa rasilimali za kununua pedi, shule imeweza kutumia sehemu ya ruzuku ya elimu kwa wanafunzi (capitation) ili kuhakikisha huduma hizi zinapatikana.

Mwalimu Mmole anaeleza kuwa shule yao imeamua kuunga mkono juhudi za wadau kwa kuhakikisha pedi na dawa za kutuliza maumivu kwa wasichana zinapatikana muda wote. Anasisitiza kuwa utekelezaji wa mwongozo wa serikali wa mwaka 2016 unaweza kuleta mafanikio makubwa iwapo wadau wote wataendelea kushirikiana. Kwa upande wake, Mwalimu Rehema Matuga, mlezi wa wasichana shuleni hapo, anasema kuwa mazingira ya shule sasa ni salama kwa wasichana na yameongeza mahudhurio yao darasani. Anabainisha kuwa awali suala la hedhi lilipuuzwa, na wasichana walikuwa wakikosa shule kwa hofu ya kukosa vifaa na faragha, lakini kwa sasa hali imebadilika na shule yao imekuwa mfano wa kuigwa.

Laya Christopher, mwanafunzi wa kidato cha nne katika shule hiyo, anaeleza kuwa tangu huduma za hedhi salama zimeboreshwa, wasichana wamekuwa na uhuru wa kuhudhuria masomo bila wasiwasi. Anaeleza kuwa uwepo wa pedi shuleni umeondoa aibu na hofu waliyoipata awali, na sasa wanaweza kuendelea na masomo yao kwa utulivu. Naye Amina Ayubu, mwanafunzi wa kidato cha kwanza, anaeleza kuwa tofauti na alivyokuwa shuleni msingi ambako suala la hedhi halikuwa likipewa kipaumbele, sasa anajisikia huru na salama kutokana na elimu anayopata na upatikanaji wa vifaa vya hedhi shuleni.

Aliyekuwa Afisa Programu wa ONGAWA katika mradi huo Bi. Leonia Andrew, anasema kuwa lengo lao ni kuboresha mazingira ya utoaji elimu kwa watoto wa kike ili waweze kumaliza elimu yao ya sekondari bila vikwazo vya hedhi. Anasisitiza kuwa viongozi wa serikali waliopata mafunzo kuhusu hedhi salama wanapaswa kuhakikisha suala hilo linapewa kipaumbele katika bajeti za maendeleo. Kaimu Afisa Mtendaji wa Kata ya Zirai, Florence Mosha, anasisitiza kuwa kila kijiji kinapaswa kuchukua hatua za dhati katika kutekeleza mpango kazi wa kuhakikisha huduma za hedhi salama zinaboreshwa mashuleni.

Shule ya Sekondari ya Zirai ina zaidi ya wasichana 150 ambao kwa sasa wanatumia boksi 10 za pedi kila mwezi. Pedi hizo zinapatikana kwa michango ya wadau mbalimbali, shule kupitia bajeti yake ya capitation, na Kituo cha Taarifa na Maarifa Zirai ambacho kinashirikiana na wadau wa maendeleo. Katika mafunzo ya uandaaji wa bajeti zenye mrengo wa kijinsia yaliyofanywa na TGNP na ONGAWA, viongozi wa vijiji vya Kwalumbizi, Zirai na Kizerui walikubaliana kuhakikisha shule za msingi katika vijiji vyao zinajengewa vyumba maalum vya kujisitiri kwa wasichana na kutenga bajeti kwa ajili ya ununuzi wa pedi. Pia wameweka kipaumbele katika ujenzi wa maeneo ya kuchomea taka (incinerators) kwa ajili ya kuteketeza pedi zilizotumika, ili kuhakikisha usafi unazingatiwa.

Hatua hizi zinathibitisha kuwa upatikanaji wa huduma za hedhi salama umeleta mabadiliko makubwa katika maisha ya wasichana shuleni, kuimarisha mahudhurio yao, na kuwafanya kushiriki masomo kwa kujiamini. Ushirikiano wa serikali, wadau wa maendeleo, walimu na jamii kwa ujumla ni msingi muhimu katika kuhakikisha kila mtoto wa kike anapata fursa sawa ya elimu bila vikwazo vya hedhi.

 









No comments:

Post a Comment