Friday, July 19, 2024

RC Singida awafunda wanawake viongozi

 RC Singida awafunda wanawake viongozi

Washiriki wa mafunzo kutoka Mikoa ya Simiyu na Singida, wakishangilia wakati wa Kumpokea Mkuu wa Mkoa wa Singida, Mhe. Halima Dendego. 


Na Deogratius Koyanga, Singida

 MKUU  Mkoa wa Singida, Halima Dendego amewataka wanawake viongozi wanaotoka kwenye vikundi vya kijamii vya uzalishaji na wakulima kujitokeza kwenye kugombea uongozi katika ngazi mbalimbali ili kuchangia kuboresha bajeti na mipango ya serikali za mitaa iweze kuzingatia mahitaji ya kijinsia.

 Akizungumza wakati wa kufunga mafunzo ya uongozi na ushiriki wa wanawake kwenye nafasi mbalimbali za uongozi zikiwemo kamati na bodi mbalimbali ngazi za vijiji na kata, yaliyoandaliwa na shirika la Helvetas-Tanzania, chini ya mradi wa Wanawake katika uzalishaji wa ukijani, mjini Singida, Dendego amesema kwamba ni lazima wanawake wajitokeze kuomba nafasi za uongozi katika maeneo yote zaidi ya siasa ili waweze kulinda uoto wa asili, mazingira na kuboresha usalama wa chakula.

 







“ Tunapokuwa na wanawake kwenye nafasi za uongozi jamii inakuwa salama, na sio kwamba wanaume wamefanya makosa au hawafanyi kazi vizuri,  wametuongoza siku nyingi tangu uhuru na mambo mazuri yametokea,  lakini sasa wanahitaji tuwasaidie pia ili  tuungane nao katika kujenga taifa hili na kuleta maendeleo ambayo ni shirikishi.”alisema Dendego.

 

Kwa upande wake, Meneja Mradi wa Ukijani, kutoka Shirika la Helvetas- Tanzania, Shoma Nangale, alisema kwamba   mradi unalenga kujenga uelewa wa washiriki, kupata ujuzi na stadi za kuwezesha kujiandaa na kuwania nafasi za maamuzi na uongozi za kuteuliwa, kuchaguliwa ama kugombea ili waweze kusimamia miradi ya maendeleo, na kuhakikisha masuala ya wanawake yanapata kipaumbele  hasa katika sekta ya mazingira, usalama wa chakula na ulinzi wa rasilimali asilia.

 

Mradi wa Ukijani  unatekelezwa katika Halmashauri tatu za Mkoa wa Singida ambazo ni Manyoni, Iramba na Ikungi na kwa Mkoa wa Simiyu ni Halmashauri za Bariadi Mji, Bariadi DC na Meatu ambapo Zaidi ya wanawake 3,000 wananufaika moja kwa moja na mradi huo. 

No comments:

Post a Comment