TGNP yawezesha viongozi wanawake na wenza wao kusimulia hadhithi za mafanikio
Na Mwandishi Wetu
Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) kwa kushirikiana na
Aghakan Foundation (AKF-T), wameendesha warsha ya Masimulizi ya hadithi za
mafanikio kwa viongozi wanawake na wenza wao ili kujadili changamoto
wanazokumbana nazo katika kutekeleza majukumu yao ya kiuongozi.
Picha ya pamoja ya viongozi wanawake na wenza wao baada ya warsha iliyofanyika katika Ukumbi wa Riverside, mjini Kondoa |
Warsha hiyo iliwahusisha Madiwani wanawake na wenza wao,
viongozi wa Kata, vijiji na Vitongoji katika Halmashauri ya wilaya ya Kondoa,
Mkoani Dodoma.
Akizungumza Mwezeshaji kutoka TGNP, Deogratius Temba,
alisema kwamba Mradi huo unalenga kujenga na kuimarisha mahusiano kati ya wenza
wa viongozi wenyewe lakini pia kuangalia
changamoto ambazo wanawake viongozi wanapitia hadi kufikia maendeleo.
“Kila kiongozi aliyepo hapa anayo mafanikio, mafanikio haya
yamekuja kwa kupitia changamoto pia, kufikia hali nzuri kuna watu wamekuwezesha
kufika hapo, labda ni Mwenza wako, jirani, mwalimu, kiongozi wa Chama chako, mwajiri,
kiongozi wa dini au yeyote. Lakini pia hadithi yako itajenga uelewa kwa wengine
na kuwatia moyo…’ alisema Temba
Washiriki wakiwa tayari kwa kusikiliza masimulizi ya hadithi za safari ya uongozi kutoka kwa viongozi wanawake |
Ameongeza kwamba, kupitia masimulizi ya hadithi, madiwani
watawapa moyo viongozi wanawake wanaotoka ngazi za chini vitongoji na vijiji
ili wasonge mbele zaidi kwani huko ndiko wanakumbana na vikwazo vikubwa vya
mila, desturi, mitazamo hasi, lakini pia majukumu ya kazi ambazo hazina malipo
(unpaid care work) yanawaelemea sana
wanawake sana wanawake viongozi na kupelekea kushindwa kutekeleza vizuri
majukumu ya kiuongozi.
Akitoa hadithi ya kukwama na kufanikiwa katika safari ya uongozi, Fatuma Iddi Issa Diwani wa Viti maalum, Halmashauri ya Kondoa Mji, alisema kwamba, pamoja na kuanza mapema safari ya kisiasa akiwa na umri wa miaka 20, hakufanikiwa kufikia lengo lake kwa wakati kutokana na kukwamishwa na watu wa karibu.
Mhe. Fatma Said Idd, Diwani wa Viti Maalum, Kondoa Mji |
“Nilitakiwa kuwa mbali sana, kama nisingekwamishwa, leo
nilitakiwa kuwa Mbunge na sio Diwani tena, lakini nilipoteza mwelekeo hapo katikati, sijakata tamaa, nasonga mbele
kwa ujasiri “ alisema Fatuma.
Kupitia mjadala na masimulizi ya hadithi, wenza wa viongozi
wanawake nao walisimulia safari za uongozi za wenza wao na jinsi ambavyo
wamewawezesha kutimiza majukumu ya kiuongozi kwa kuwasaidia baadhi ya kazi za
nyumbani kama kulea watoto, kuandaa chakula, kuvua, kusafisha shamba na kutunza
mifugo.
Mwezeshaji kutoka TGNP, Deogratius Temba |
Katika simulizi za safari ya uongozi kwa viongozi wanawake
waliohudhuria, wenza wao walitoa ushuhuda jinsi ambavyo walichangia wake zao
kufikia hatua hiyo, ikiwepo, kuwashawishi, kuwawezesha kifedha, rasilimali
nyigine lakini pia kuwapa muda wa kutekeleza majukumu.
No comments:
Post a Comment