Na Mwandishi Wetu, Arusha
Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP)
inashiriki maadhimisho ya wiki ya Asasi za Kiraia (CSO) inayofanyika Jijini
Arusha kwa kutoa elimu juu ya umuhimu ya wajamii kushiriki kwenye ubunifu wa
kisayansi na Kiteknolojia kwa kuzingatia usawa wa Kijinsia kwa maendeleo
Endelevu.
Mkutano wa wahandishi wa Habari na Kamati ya Maandalizi ya Wiki ya CSOs uliofanyika leo jijini Arusha |
Maadhimisho ya Wiki ya CSOs yanayotarajiwa kuanza kesho Oktoba 23, 2023 Jijini Arusha yatahusisha asasi za kiraia Zaidi ya 500, kutoka mikoa yote ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na nchi jirani, huku kukiwa na mada mbalimbali ambapo mada kuu inalenga ushiriki wa asasi za kiraia katika Teknolojia katika kufanikisha shughuli zake za kitoa huduma kwa jamii nchini, na Zaidi kutafakari mafanikio ya nyuma, ya sasa na ya baadaye sambamba na changamoto zake.
Akizungumza Mwakilishi wa TGNP
katika Mkutano na wandishi wa Habari leo uliowahusisha wakurugenzi wa mashirika
mbalimbali na kamati ya kitaifa ya uandaaji wa maadhimisho hayo, Deogratius
Temba, alisema kwamba, pamoja na TGNP kushiriki kwenye shughuli zote, kwa
kushirikiana na mashirika mengine, pia wataendesha warsha na majadiliano ambayo
yataangazia Ubunifu na uvumbuzi wa
kiteknolojia kama chachu ya usawa wa Kijinsia.
Temba ameeleza kwamba, mada hiyo
itawahusisha wadau mbalimbali, mashirika, wanazuoni na wataalamu wanawake na wasichana walio kwenye Ubunifu na uvumbuzi
wa kiteknolojia katika kuondoa changanmoto zinazoikumba jamii hasa wanawake na
watoto.
“Tutakuwa na wanafunzi wasichana kutoka
DIT ambao ni wavumbuzi wa kiteknolojia, wanaolenga kuondoa changamoto za
kijamii katika taifa letu. TGNP tumejenga uwezo kwa jamii na taasisi mbalimbali
kubomoa mifumo kandamizi na mitazamo hasi juu ya uwezo na ushiriki wa wanawake
hasa wasichana katika Sayansi, Teknolojia, na Hisabati, sasa wapo wasichana
wanaofanya vizuri kwenye ngazi ya vyuo vikuu kama Taasisi ya Teknolojia Dar es
salaam (DIT), wamefanya vizuri sana,” alisema Temba na kuongeza:
“Ukiangalia kwa hapa tulipofikia
kama nchi, tumepiga hatua, vifaa vipo,lakini bado kuna pengo la usawa wa
kijinsia na ushiriki au ujumishwaji wa makundi yote, tunachofanya kwa
kushirikiana na Taasisi mbalimbali ni kubadilisha mitazamo hasi, lakini pia
kushaiwshi serikali kutenga bajeti ya kutosha kwenye TEHAMA hasa mashuleni, na
kuondoa au kuunguza kodi kwa vifaa hivyo ili watoto waweze kujifunza na
kuonesha ubunifu wao” alisema Temba.
Aidha, amesema kwamba, Nchi kama
Tanzania zinaweza kufaidika sana na kuendeleza sera na mipango inayowezesha ushiriki
wa wanawake katika sekta ya teknolojia na kuhakikisha kwamba teknolojia
inatumika kwa njia inayolinda usawa wa kijinsia. Hii inaweza kuchangia katika
maendeleo ya kijamii na kiuchumi na kuboresha hali ya maisha kwa wanawake na
wanaume kwa usawa.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa
Kamati ya Maandalizi ya wiki ya CSO
Niensia Mahenge alisema kwamba, Teknolojia inatoa fursa kwa wasichana na wanawake kupata elimu
na kukuza ujuzi. Majukwaa ya kujifunza mtandaoni, programu za elimu, na
rasilimali za kidijitali huwezesha kujifunza kwa umbali na kujifunza bila
shinikizo la muda, kupunguza vikwazo vya kuingia.
“Teknolojia inaweza kuboresha
upatikanaji wa huduma za afya kwa wanawake, hasa katika maeneo yasiyopewa
kipaumbele. Huduma za tiba kwa njia ya mtandao na programu za afya za simu
hutoa zana kwa wanawake kudhibiti afya na ustawi wao, ikiwa ni pamoja na huduma
za ujauzito, uzazi wa mpango, na usaidizi wa changamoto za kiafya” alisema
Mahenge.
Hata hivyo, wadau wameshauri
kwamba ni muhimu kuzingatia kuwa
teknolojia na uvumbuzi pia yanaweza kuwa na athari hasi kwa usawa wa kijinsia
ikiwa haitazingatia changamoto za kijinsia na inaweza kuongeza pengo la
kidijitali. Kwa mfano, wanawake wengi katika nchi za dunia ya tatu wanaweza kukosa
upatikanaji wa vifaa vya teknolojia au elimu ya kutosha ya kidijitali. Kwa
hiyo, juhudi zinahitajika ili kuhakikisha kwamba teknolojia na uvumbuzi
unawafikia wanawake na wanaume sawa na kuchangia katika kuboresha usawa wa
kijinsia.
No comments:
Post a Comment