· * Watumishi
wa afya wanaoishi kwenye wodi ya wazazi kuhamishwa
· * Changamoto
ya maji kwenye zahanti yaibuliwa
· *Uongozi
wa Vijiji kusimamia vichomea taka zahanati
Na Deogratius Temba, Kondoa
WATUMISHI wa zahanati ya Kijiji cha Mafai,Kata ya
Haubi, Wilaya ya Kondoa wanaoishi katika
wodi zilizojengwa kwa ajili ya huduma ya mama na mtoto, wametakiwa kutafuta nyumba
za kuishi ili kupisha wodi hizo kutumika kwa lengo husika.
Akizungumza wakati wa kujibu hoja
zilizoibuliwa kwenye zoezi la Uwajibikaji na Ufuatiliaji wa Jamii (SAM) kwa
mtazamo wa Kijinsia, lililoendeshwa na Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), katika sekta ya afya, Kaimu Mkurugenzi
Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kondoa,Mashauri Visenti, alisema kwamba
watumishi wa zahanti ya Mafai, ambao wanaishi kwenye wodi za Mama na Mtoto
wanapaswa kuhamia kwenye nyumba za kupanga kijijini ili kupisha huduma ya mama
na mtoto kuendelea katika vyumba hivyo kwa ufanisi zaidi ikiwa ni pamoja na
kuhakikisha usalama wa vifaa vilivyopo kwenye zahanati hiyo.
![]() |
Timu ya SAM ikiwa nje ya Jengo la zahanati ya Mafai, ilipotembelea kuona ubora wa utoaji wa huduma za afya |
“kwa sababu sasa tumeshatimiza
mwaka mmoja tangu kuanza kazi kwa zahanati hii, tunashauri, wapishe zile wodi
ili kuboresha Zaidi huduma ya mama na mtoto katika zahanati yetu ile..” alisema
Mashauri.
![]() |
Timu ya SAM ikiendelea na uchambuzi na mapitio ya nyaraka mbalimbali za Halmashauri ya Kondoa DC kwa muda wa siku tatu |
Awali akizungumzia jambo hilo,
Katibu wa Afya wilaya ya Kondoa, alisema kwamba, awali watumishi hao walikuwa
wapya, na ndio walipelekwa kwa ajili ya kuanzisha zahanati hiyo mpya, wakaomba
kuishi kwenye vyumba hivyo vya zahanati ili waweze kuzoea mazingira na kutafuta
vyumba katika kijiji hicho.
“sasa wamezoea, mazingira, na
wameshakaa Zaidi ya mwaka, awali tuliwaruhusu kwa sababu ndio walikuwa wanaenda
kuanza kazi katika kijiji kile, tutawa andikia barua ya kuwataka kutafuta
nyumba kijijini ili waweze kupisha huduma ziendelee pale. Pia sio salama kiafya
kwa wahudumu kuishi ndani ya Hospitali au vyumba vya matibabu.” Alisema Mbaga.
Awali akiwasilisha matokeo ya SAM
kwa wadau wa Halmashauri pamoja na Menejimenti, Mwezeshaji wa SAM kutoka
Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) Deogratius Temba alisema kwamba, pamoja na
changamoto ambazo zilioonekana za kibajeti, na utoaji wa huduma za afya kwa
kuzingatia usawa wa Kijinsia, Halmashauri ya wilaya ya Kondoa imejitahidi
kutenga bajeti ya afya kwa mrengo wa kijinsia ikiwa ni pamoja na kupata hati
safi kwa mujibu wa ripoti ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) ya mwaka 2021/2022.
![]() |
Mwezeshaji Deogratius Temba, kutoka TGNP akitoa mafunzo mafupi maana ya SAM kwa mrengo wa Kijinsia, umuhimu wake na maeneo Muhimu ya Kijinsia ya kufuatilia |
Temba aliishauri halmasahuri kuweka
uzito na umuhimu katika maeneo ambapo kuna vifaa tiba vya mama na mtoto vitumike na kutunzwa. Mfano, zahanati ya Mafai,
wahudumu wanatumia vyumba vya wodi ya mama na mtoto kwa malazi, chumba kinachotumika
kwa sasa kama wodi na chumba cha kujifungulia (labor Room) kipo eneo la
wazi karibu na ukumbi wa OPD. Hakuna
usiri wala faragha Kwa mama anayejifungua.
“ ..Kutokana na kutokutumika kwa
wadi ya mama na mtoto iliyonjengwa kwa kazi hiyo, uhifadhi na utunzaji wa vifaa tiba na mashine za
kisasa zilizonunuliwa kwa ajili mama na
mtoto unakuwa dhaifu. Mfano mashine
nzuri za Oxygen, kuvuta uchafu kwenye pua za watoto wachanga (suction machine)
na sterilizer ya kisasa vilikutwa chini kwenye sakafu” alisema temba na
Kuongeza:
“ Hatukuona bajeti kwa ajili ya Zahanati ili kuhakikisha zinapata
maji safi na salama kwa ajii ya mahitaji ya kina mama wanaojifungua. Hata tulipoitembelea
Zahanati ya Mafai kisima kilichopo jirani hakijaanza kutumika, lakini pia kina
mama wanaojifungulia zahanati hawana huduma ya maji….” Alisema Temba
Aidha timu ya SAM kwa mrengo wa
Kijinsia iliishauri Halmashauri kutenga bajeti kwa ajili ya nyumba za watumishi kwani
kuna maboma ya nyumba za watumishi wa kada ya afya ambazo zimejengwa na jamii
kwa nguvu zao, lakini zipo hatua ya lenta muda mrefu. Mwaka wa fedha 2021/2022
hakuna bajeti iliyotengwa kwa ajili ya nyumba za watumishi wa afya huko
vijijini, Mfano jengo nyumba ya
watumishi Zahanati ya Mafai ambalo limejengwa na wananchi hadi hatua ya lenta
tangu mwaka 2014, sasa limeanza kuharibika.
![]() |
Zoezi la SAM na mafunzo yake liliendeshwa kwa njia shirikishi za kiraghibishi ili kujenga uelewa wa pamoja |
Naye Diwani wa Kata ya Haubi,Paulo
Irovya, ambapo zahanati hiyo, ipo
alisema kwamba ataitisha Kikao cha Kamati ya Maendeleo ya Kata (WDC) ili kuweka
mikakati ya kukabiliana na changamoto zilizo onekana katika zahanati hiyo, hasa
zilizo ndani ya uwezo wao badala ya kusubiria bajeti ya Halmashauri ambayo
wakati mwingine haitoshi kutatua changamoto zote za jamii.
Katika kikao hicho, Mwenyekiti wa
Kijiji cha Mafai, Mursal Juma Doiyya, aliahidi kuitisha mkutano wa kijiji na kuwahamasisha
wanakijiji kujenga kichomea taka katika zahanati hiyo, sambamba na kuendeleza
ujenzi wa nyumba ya wahudumu ambayo imeishia hatua ya lenta ambayo inauwezo wa
kutumika na familia mbili.
Mashine maalum ya kuchemshia vifaa tiba, ikiwa chini sakafuni kwenye chumba cha kujifungulia |
No comments:
Post a Comment