Na Deogratius Temba, Kibaha
Wananchi kutoka kata ya Pangani, Halmashauri
ya Wilaya ya Kibaha Mji, wanaoshiriki utafiti wa kiraghibish unaofanywa na
Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), wametoa mapendekezo yao 11, yanayotokana na changamoto
zilizoibuliwa wakati wa zoezi hilo lililoanza mapema mwezi huu
![]() |
Picha ya pamoja ya washiriki wa kikao kazi cha mrejesho wa utafiti raghibish ngazi ya Halmashauri, uliofanywa na TGNP , katika Halmashauri ya Kibaha Mji |
Kikao kazi hicho cha mrejesho ngazi ya Halmashauri ni sehemu ya utekelezaji wa Mradi wa “ Uimarishaji wa Sauti za wanawake, wasichana na watu wenye ulemavu katika uongozi na haki ya kumiliki rasilimali” unaofadhiliwa na Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia masuala ya wanawake (UNwomen).
Washiriki hao, wakiwasilisha
mapendekezo yao kwa Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Mji wa Kibaha, Charles
Marwa, wamesema kwamba, pamoja na mapendekezo hayo, pia wameandaa mpango kazi
ambao watautekeleza sambamba na viongozi wao. Kikao kazi hicho kilichoandaliwa
na Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) kwa kushirikiana na Idara ya Maendeleo ya
Jamii wilayani hapo, pia kimehudhuria na wakuu wa Idara na Vitengo wa
Halmashauri hiyo.
“Kutokana na hayo hapo juu, kutokana
na changamoto kubwa zilizoibuliwa ambazo ni Uongozi usiowajibika na
usiozingatia uwakilishi wa Kijinsia, Mila na desturi kandamizi, umiliki wa
ardhi na rasilimali nyingine na Ukatili wa kijinsia hasa mimba za utotoni. Biashara haramu ya ngono inachochea
mmomonyoko wa maadili, na kuongeza matukio
ya Ubakaji kwa wanawake hasa wasichana, kuongezeka kwa uporaji na migogoro
mikubwa ya ndoa ambayo inaadhiri kwa kiasi kikubwa watoto” amesema mwasilishaji
wa mapendekezo hayo”alisema mwasilishaji.
Tunapendekeza yafuatayo kwa
ujumla wake yafanyiwe kazi.
- Kutokana
na suala la uongozi usiowajibika kuibuka, na kukosekana kwa uwakilishi wa
Kijinsia katika uongozi, na kupelekea kukosekana kwa sauti za wanawake,
wasichana na watu wenye ulemavu kwenye maamuzi. Elimu ya usawa wa kijinsia
itolewe kwa viongozi walioko madarakani, viongozi wa vyama vya siasa
kuanzia ngazi za chini hadi wilaya.
- Viongozi
walioko madarakani katika mitaa, wajengewe uwezo ili kujua mipaka ya
kiutendaji, uwajibikaji, uandaaji wa miradi ya maendeleo kwa kuzingatia
vipaumbele vyenye mtazamo wa Kijinsia, ushiriki wa wananchi kwenye
mchakato wa O&OD
- Halmashauri
isimamie mchakato wa uandaaji wa bajeti uwe shirikishi kuanzia ngazi za
mitaa ili kuwepo kwa bajeti yenye mrengo wa Kijinsia itakayogusa mahitaji
ya kila kundi na kuwezesha wanawake kumiliki rasilima.
- Halmashauri
kwa kushirikiana na TARURA izipe kipaumbele barabara zinazounganisha Kata
ya Pangani na Mji wa Kibaha ili kurahisisha usafiri na kupunguza kiwango
cha umasikini kwa jamii na
kupunguza vifo vya mama na mtoto.
- Mwaka
wa fedha 2024/25, Halmashauri itenge bajeti kwenye mapato yake ya ndani,
kwaajili ya kugharamikia urasimishaji wa ardhi na mipango miji ili
kupunguza mzigo wa gharama kubwa za upimaji kwa wananchi hasa wanawake na
watu wenye ulemavu, lakini pia fedha hizo zitarudi kupitia kodi
itakayolipwa baada ya kumilikishwa.
- Kuhuisha
kamati za Ulinzi wa Mama na Mtoto (MTAKUWWA) katika kata na Mitaa yote,
zitambue majukumu yake na mfumo wa uwajibikaji yaani ziwe na taarifa zake
za utekelezaji.
- Bado
tuna kundi la wanawake wasiojua kusoma na kuandika katika kata ya pangani.Tunashauri
kuondoa tatizo hili mwongozo wa kuwarudisha
wanafunzi walioacha masomo kwa
sababu mbalimbali uanze kutumika ndani ya Kata ya Pangani. Mratibu Elimu
Kata (MEK) aanze kuwabaini wasichana walioko mitaani na kuwarudisha
shuleni kwa mujibu wa mwongozo au waraka wa Elimu namba 1 wa mwaka 2022.
- Halmashauri
isaidie usimamizi na utekelezaji wa
sheria ndogo ambazo zitathibiti watoto wa shule kuzurura hovyo mitaani, kila
shule itoe huduma ya chakula kwa wanafunzi, watoto kutokushiriki ngoma na
mikesha ya usiku ya ngoma, kufunga sehemu zote zenye ‘ubanda’
panapofanyika biashara haramu ya ngono na mabanda mengine ya kuonyesha
video yadhibitiewe watoto wasiingie.
- Sheria
kali zichukuliwe dhidi ya kutokomeza Mimba na ndoa za utotoni. Maafisa
Ustawi wa jamii na Maendeleo ya jamii washirikiane na dawati la Jinsia na
Mtoto-Polisi, kuharakisha kesi za ubakaji na wanaobainika wahukumiwe kwa
mujibu wa sheri zetu.
- Kutenga
bajeti kwaajili ya kupeleka maji kwa mitaa sita (6) kati ya Minane (8), ya
Kata ya Pangani ambayo haina maji kabisa, hii inapelekea kuongezeka kwa
vitendo vya Ukatili wa Kijinsia
- Katika
uibuaji, kulijitokeza tatizo la kukidhiri kwa rushwa ya pesa na rushwa ya
ngono ili kupata huduma, hasa urasimishaji wa ardhi. Tunashauri, viongozi
wa serikali za Mitaa wajengewe uwezo ili wazingatie uadilifu, maadili ya
uongozi na utawala bora.
No comments:
Post a Comment