* Shule ya wasichana ya Galijembe yaongoza kimkoa
*Halmashauri yaanza ujenzi wa shule nyingine ya wasichana, kufunguliwa 2024
*Mpango wa Chakula mashuleni wasisitizwa
*Halmashauri yaendelea kutenga bajeti kwa taulo za kike mashuleni
Na Deogratius Temba,
Mbeya
Mafunzo ya Elimu ya Uandaaji wa Bajeti yenye mrengo wa kijinsia
kwa watendaji wa Halmashauri, Madiwani na jamii yamefanikisha mageuzi makubwa
ya kielimu katika halmashauri ya wilaya ya Mbeya.
Mafunzo, semina na warsha mbalimbali ambazo zimekuwa zikifanywa
na Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) tangu mwaka 2013 kwa viongozi wa
halmashauri na jamii kupitia vituo vya taarifa na maarifa imechangia Halmashauri
kuona umuhimu wa watoto wa kike kupata elimu bora kwa kuweka mazingira salama
na yenye kuvutia ili wasichana wapate elimu nzuri.
Akizungumza na Mwandishi wetu, Mwenyekiti wa halmashauri ya
wilaya ya Mbeya Mwalingo Kisemba, amesema kwamba kutokana na elimu iliyotolewa
na kujnegwa uwezo juu ya masuala ya Kijinsia, viongozi wa Halmashauri waliona
umuhimu wa kuwa na shule maalum za wasichana na zenye mazingira salama ili
kuongeza idadi ya wasichana wanaomaliza kidato cha nne na kufaulu vizuri na
kuondoa changamoto za kijinsia zilizokuwa zikichangia utoro na mimba za utotoni
kwa wasichana.
![]() |
Picha ya Waraghibishi / wakufunzi wa bajeti yenye mrengo wa Kijinsia Dr. Geofrey Chambua na Deogratus Temba, walipoitembelea shule hiyo mwaka 2021. |
“Sisi baada ya kujengewa uwezo, tulitambua umuhimu wa mtoto
wa kike kupata elimu, lakini tukakubaliana ndani ya halmashauri kwamba tuweke
mikakati ya kupata shule nzuri. Lakini wananchi wa kata hizi nao walikuwa
wameshapata uelewa wa elimu hii kupitia TGNP, waliweza kutusaidia kuhamasishana
na kukubaliana kutoa nguvu kazi na michango yao na kuweza kuijenga shule ya
Galijembe.” Alisema Mwenyekiti.
Anaongeza kwamba, TGNP ilifika Mbeya Zaidi ya miaka 10
iliyopita, wazo hili lilikuwa bado, lakini kutokana na uchechemuzi uliokuwa
unafanyika baada ya uraghibishi na kuanzishwa kwa vituo vya taarifa na Maarifa,
wa kudai uwepo wa shule karibu na makazi ya watu ili kupunguza umbali kwa
wasichana wanaotembea kwenda shule na kukumbana na vishawishi njiani na kupata
ujauzito, wananchi wa kata za Tembela na Ijombe walifuatilia kwa mamkala za
serikali ngazi ya Halmashauri, na kuwezesha kuchokoza wazo hilo kuibuliwa na
kuanyiwa kazi pamoja na kwamba lilichukua muda mrefu.
![]() |
Baadhi ya majengo ya shule ya sekondari ya wasichana ya Galijembe, Mbeya DC hiyo yanavyoonekana kwa sasa. |
Kwa upande wake, Makamu Mkuu wa Shule ya wasichana ya
Galijembe, Mtango Nimziaeli, alisema kwamba shule hiyo ilianzishwa mwaka 2019,
ikiwa na wanafunzi 50 na walimu watato (5) ambao sasa wapo walimu 25 wakiwemo
wa kike saba (7) na wa kiume 18.
Alisema kwamba, shule hiyo licha ya kwamba imechukua
wanafunzi wenye ufaulu wa kawaida tu kwa shule za msingi za Halmashauri hiyo,
matokeo ya kidato cha nne kwa mwaka 2022 ufaulu ni wa juu na wa kuridhisha
kwani shule imekuwa ya kwanza kimkoa, ikiwa na ufaulu wa madaraja kama
ifuatavyo; daraja la kwanza 20, la pili 20 na la tatu 10, ambapo hakuna daraja
la nne wala sifuri.
![]() |
Mwenyekiti wa Halmashauri Mwalingo Kisemba, akiwa na Walimu pamoja na wageni kutoka TGNP waliotembelea shuleni hapo hivi karibuni |
Mwalimu Mtango alisema kwamba wanafunzi waliofaulu vizuri pia
walifanya vizuri masomo ya sayansi na wengi wao wamepangwa kusomea michepuo ya
sayansi kwa kidato cha tano na wengine wataenda vyuo vya kati kusomea kozi za
sayansi.
Akizungumzia siri ya mafainikio ya shule hiyo, Mwalimu Mtango
alisema: “…ni jitihada za waalimu tu, Mkuu wa shule anajitahidi sana kujenga
timu imara na kupanga safu yake vizuri, kuna kutiana moyo, kila mwalimu
anajitahidi vya kutosha.
“kuna wakati hata uongozi unashangaa jinsi ambavyo waalimu
wanajitahidi, kila mmoja ana moyo na kazi, waalimu wapo tayari kuchelewa kutoka
shuleni au kuwahi hapa shuleni ili kuwandaa wanafunzi kwa mitihani. Ni timu ya walimu ambayo kwa kweli imejitoa, wanajituma kiukweli, tuna bahati ya kuwa na timu hii ya
waalimu, kila mmoja anaipenda kazi yake na anawajibika kwa kiwango cha juu,
ndio maana tumepata haya matokeo mazuri” alisema Mwalimu Mtango.
Lakini pia, Mwalimu huyo aliongeza kwamba, uzalendo kwa
Halmashauri pia umechangia kwani kila mwalimu anaiona shule kwamba ni taasisi
ya halmashauri na ni lazima ailetee Halmashauri heshima.
Mwenyekiti wa Halmashauri alisema kwama, kipaumbele cha halmashauri ni Elimu, na wataka kuona kila mwananchi wa Halmashauri anaelewa dhana hiyo, na lengo ni kuhakikisha watoto wa kike wanafaulu vizuri na wanatimiza ndoto zao.
Anaongeza kwamba: “ hata ukiangalia miundombinu ya shule,
tumezingatia mahitaji maalum ya wasichana, vyumba maalum vya kubadilishia
wakati wa hedhi vipo, taulo za kike kila mara tunawapatia, na tumeweka kwenye
bajeti ya Halmashauri, tunaendelea kuzingatia mahitaji ya kisera kwa uwiano wa
matundu ya vyoo kwa shule zetu kuhakikisha matundu ya vyoo yanaongezeka.”
Pia aliongeza kwamba, kati ya shule 152 za msingi kwa halmashauri
hiyo, Zaidi ya asilimia 85 ya shule
wanafunzi wanapata chakula ili kupunguza utoro.
“nimesema kila mara na madiwani wenzangu na wataalamu wetu
kwamba, halmashauri hii sitaki kuona utapia mlo, nataka watoto wasome vizuri na
wapate ufaulu, kwahiyo hapa Mbeya sisi hatuna shida ya chakula au nafaka, kila
mzazi ni lazima atoe au kuchangia chakula shuleni ili watoto wakue vizuri na
kufaulu masomo” alisema Kisemba.
Alisema kwamba, kutokana na uelewa sasa wa masuala ya usawa
wa Kijinsia, na jinsi ambavyo TGNP imeendelea kuweka nguvu ya kujenga uwezo kwa
jamii kupitia vituo vya taarifa na
maarifa, wananchi walichangia ujenzi wa shule hiyo, na sasa wanachangishana
kujenga shule nyingine ya wasichana inayoitwa shule ya Sekondari ya wasichana
ya Pareto, Ilembo, tarafa ya Isagati (Pareto Girls Secondary school) ambayo
wamewaomba wadau wa pareto kuchangia pia.